Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, ametembelea banda la Bodi ya Usajili wa Wataalam wa Mipangomiji (TPRB) katika Maonesho ya Kimataifa ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam, na kujionea huduma mbalimbali zinazotolewa na bodi hiyo kwa wananchi na wadau.
Akiwa katika banda hilo la TPRB, Waziri Akwilapo alipokea maelezo kutoka kwa wataalamu wa TPRB, kuhusu huduma zinazotolewa na Bodi hiyo katika maonyesho hayo, zikiwemo utoaji wa elimu ya mipangomiji, ushauri wa kitaalamu pamoja na usajili wa wataalamu na kampuni zinazojihusisha na shughuli za mipangomiji.

Dkt. Akwilapo ameipongeza TPRB kwa jitihada za kusogeza huduma karibu na wananchi, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kutoa huduma bora na elimu kwa umma kuhusu shughuli zinazofanywa na Bodi hiyo.
Awali, Kaimu Msajili wa TPRB, TP. Martha Mkupasi alisema kuwa Bodi hiyo imejipanga kuhakikisha wananchi wanapata elimu ya masuala ya mipangomiji pamoja na huduma za kitaalamu kwa urahisi zaidi kupitia banda lao.Kwa mujibu wa TP.
Mkupasi, huduma hizo zinazotolewa kwenye banda hilo zimekuwa na mchango mkubwa katika kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu umuhimu wa mipangomiji na kurahisisha upatikanaji wa taarifa muhimu, huku akiwakaribisha wananchi na wadau mbalimbali kutembelea banda hilo ili kunufaika na huduma zinazotolewa.

Kaimu Msajili huyo wa TPRB amesema Bodi hiyo inaendelea kutoa huduma mbalimbali katika banda lake la maonyesho Sabasaba, ikiwemo elimu ya mipangomiji, ushauri wa kitaalamu, pamoja na huduma za usajili kwa wataalamu na kampuni zinazojihusisha na shughuli za mipangomiji pamoja na kupokea kero mbalimbali kutoka kwa wananchi na kuzifanyia kazi.



