Na Tatu Mohamed
BODI ya Utalii Tanzania (TTB) imesema imeanzisha dawati maalumu katika Maonesho ya 50 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (Sabasaba) kwa lengo la kutoa elimu kwa wananchi na wadau kuhusu Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Swahili International Tourism Expo (SITE) 2026.
Akizungumza katika maonesho hayo, Afisa Masoko wa TTB, Abdilahi Ameir, alisema dawati hilo linatumika kuhamasisha wananchi na wadau kushiriki maonesho ya SITE pamoja na kuwafahamisha kuhusu fursa mbalimbali zilizopo katika sekta ya utalii.

Amesema SITE ni maonesho ya kimataifa yanayowakutanisha wadau wa biashara ya utalii na wanunuzi wa huduma za utalii kutoka mataifa mbalimbali duniani kwa lengo la kukuza biashara na kuitangaza Tanzania kama kitovu cha utalii.
Kwa mujibu wa Ameir, maandalizi ya SITE 2026 yanaendelea vizuri, huku zaidi ya wanunuzi 50 wa huduma za utalii kutoka nchi mbalimbali, ikiwemo Korea, Urusi na nchi za Ulaya Mashariki, wakiwa tayari wamethibitisha ushiriki wao.
Aidha, alisema wananchi wa kawaida hawajaachwa nyuma kwani kutakuwa na bustani maalumu ya wanyama pori itakayowapa fursa ya kujifunza na kujionea vivutio vya utalii vilivyopo nchini.

Ametoa wito kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki Maonesho ya Swahili International Tourism Expo yatakayofanyika kuanzia Julai 23 hadi 25 katika Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam, ili kujionea fursa mbalimbali za biashara na uwekezaji katika sekta ya utalii.


