Na Tatu Mohamed
Tanzania ipo katika hatua za awali za mchakato wa kuanza uzalishaji wa umeme wa nyuklia, huku ikikamilisha maandalizi muhimu na kusubiri tathmini ya wataalamu wa kimataifa itakayobaini kiwango cha utayari wa nchi kuingia rasmi katika awamu ya kwanza ya utekelezaji wa mradi huo.
Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Nguvu za Atomiki Tanzania (TAEC), Prof. Najat Kassim Mohammed, amesema tayari tume hiyo imewaalika wataalamu wa kimataifa kufanya tathmini ya utayari wa Tanzania, na endapo ukaguzi huo utaridhisha, nchi itaruhusiwa kuendelea na hatua inayofuata ya utekelezaji wa mradi huo.

Amesema maandalizi yanayoendelea kwa sasa yanajumuisha kuimarisha mfumo wa sheria, sera na taasisi zitakazosimamia matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia kwa kuzingatia viwango vya kimataifa.
Prof. Najat amesema Serikali inalenga ndani ya kipindi cha takribani miaka saba kufikia hatua ya kuzalisha umeme wa nyuklia, hatua itakayosaidia kuongeza upatikanaji wa nishati ya uhakika kwa ajili ya kukuza uchumi na maendeleo ya sekta ya viwanda.
Aidha, amewahakikishia wananchi kuwa hakuna sababu ya kuwa na hofu kuhusu mradi huo, akieleza kuwa hatua zote za maandalizi na utekelezaji zitazingatia viwango vya kimataifa vya usalama vinavyolenga kulinda afya za wananchi na mazingira.

Akizungumzia upatikanaji wa malighafi, amesema Tanzania ina akiba ya madini ya urani, lakini madini hayo hayawezi kutumika moja kwa moja bila kupitia mchakato maalumu wa uchakataji.
Amefafanua kuwa katika hatua za awali, urani itachimbwa nchini kabla ya kusafirishwa katika nchi zenye teknolojia ya kuichakata, ikiwemo Urusi, ili kutengenezwa mafuta ya nyuklia ambayo yatarejeshwa nchini kwa ajili ya kuzalisha umeme.
Prof. Najat amesema mradi wa kwanza wa uchimbaji wa urani unatarajiwa kuanza katika eneo la Mkuju mkoani Ruvuma, huku tafiti zikiendelea katika maeneo mengine nchini kubaini uwepo wa akiba zaidi ya madini hayo.
Aidha, ametoa wito kwa wananchi kujenga uelewa sahihi kuhusu teknolojia ya nyuklia na kuondoa hofu isiyo na msingi, akisisitiza kuwa matumizi ya nishati hiyo yatachangia maendeleo ya taifa bila kuhatarisha usalama wa wananchi wala mazingira.


