SERIKALI Mkoani Katavi imeagiza kufanyika kwa uchunguzi kuhusu tuhuma za mfungwa kumbaka
mtoto mwenye umri wa miaka 13, mkazi wa Kijiji cha Kawanzinge, wilayani Mpanda.
Mkuu wa mkoa wa Katavi, Mwamvua Mrindoko amesema serikali itahakikisha muhusika wa tukio hilo anachukuliwa hatua za kisheria pasipokujali taasisi anakotoka, huku akimwagiza Kamanda wa Polisi wa mkoa huo [RPC],
Kaster Ngonyani kulifanyia kazi kwa kushirikiana na Jeshi la Magereza.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, baadhi ya vyombo vya habari viliripoti tukio la mtoto huyo alifanyiwa kitendo cha ubakaji na mfungwa wa Gereza la Kalilankulukulu Wilaya ya Tanganyika, wakati akitoka kupanda mpunga.
Tukio hilo linadaiwa kutokea Ijumaa Machi 1, 2024 saa 11 jioni katika maeneo yanayopakana na mbunga za Gereza la Kalilankulukulu ambalo ni maarufu kwa kilimo cha mpunga.
Inadaiwa kuwa mfungwa aliyefanya kitendo hicho alikuwa akichunga ng’ombe katika eneo ambalo binti aliyebakwa na watoto wenzake walikuwa wakipita kwa miguu kutoka shambani.
Inadaiwa kuwa aliwarisha watoto hao kisha kumkamata kwa nguvu binti huyo na kuingia naye vichakani na kumfanyia unyama huo.
Mtandao wa TimesMajira Online ulimnukuu binti huyo akisema mtuhumiwa huyo alimpinga ngwara, kisha alimfunga na sweta aliyokuwa nalo usoni na kuanza kumbaka na kwamba licha ya kupiga kelele, hakujali.
“Alipomaliza kunifanyia unyama huo aliniuliza nina kiasi gani cha fedha ili aniachie, nilimwambia nina shilingi 2,000 ambazo alizichukua,” anasema binti huyo.
Baba mzazi wa mtoto huyo [jina tunalihifadhi] anasema binti yake huwa na kawaida ya kuondoka asubuhi kwenda kufanya vibarua kwenye mbuga za mpunga na kurejea jioni, lakini siku ya tukio alirejea saa tatu usiku.
Anasema kuchelewa kwake kulitia hofu yeye na mkewe, hivyo waliamua kwenda kumfuatilia kwa watoto wenzake walioondoka naye na kwamba mmoja wa watoto hao ndiye aliwaambia kuwa mwenzao amebakwa na mfungwa.
Anasema walikwenda kutoa taarifa kwa Mwenyekiti wa Kijiji ambaye alimpigia simu Kaimu Mkuu wa Gereza, na mkuu huyo alimjibu kuwa malalamiko hayo yalikuwa tayari yamefikishwa gerezani hapo.
“Tukiwa tumekaa hapo kwa muda mrefu kidogo, mtoto wangu alifika hapo kwa mwenyekiti na hapo alieleza jinsi alivyobakwa, ndipo tuliamua kutoa taarifa kwenye kituo cha Polisi cha Kata ya Kakese.
Polisi wa hapo walitwambia twende moja kwa moja kwenye kituo cha Polisi cha Wilaya ya Mpanda na kisha tulimpeleka hospitali ya Manispaa ya Mpanda,” anaeleza Baba wa mtoto huyo.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Mpanda Dk.Limbu Mazoya anathibitisha Hospitali yake kumpokea mtoto huyo na kwamba baada ya kufanyiwa uchunguzi ilithibitika kuwa amebakwa.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Kawanzinge, Emanuel Machela akisema yeye alipata taarifa za mtoto huyo kubakwa siku hiyo saa tatu usiku, kisha
alimpiga simu Kaimu Mkuu wa Gereza ambaye na alimweleza kuwa wananchi wa kijiji chake walifika gerezani hapo kutoa taarifa za tukio hilo, lakini aliwambia warejee kijijini kwa sababu hawakuwa na uthibitisho.
“Baada ya wananchi kurejea hapa kijijini, kijana mmoja [jina tunalihifadhi] aliyekuwa na binti huyo, katika maelezo yake alisema walipokwenda kwenye gereza hilo kutoa taarifa, mtoto huyo alipimwa kwenye zahanati ya gereza na kuonekana amebakwa, kisha alipewa dawa,” anasema Machela.
Kaimu Mkuu wa Gereza la Kalilankulukulu analiyetambulika kwa jina la Bosco alisema hana mamlaka ya kuzungumzia suala hilo bali Mkuu wa Gereza ambaye wakati huo hakuwepo.
Kabla ya Mkuu wa Mkoa kutoa maelekezo, siku moja baada ya tukio Mtandao wa TimesMajira Online ulimtafuta Kamanda Ngonyani ambaye kupitia simu yake ya kiganjani alisema hakuwa amepata taarifa za tukio hilo, licha ya kwamba mwathirika alikuwa amepewa PF3 na polisi.