Na Mwandishi Wetu
Bodi ya Usajili wa Wataalam wa Mipangomiji (TPRB) imeendelea kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi na wadau katika Maonesho ya Kimataifa ya Sabasaba yanayoendelea jijini Dar es Salaam.
Katika banda la TPRB lililopo ndani ya Banda la Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bodi imejikita katika kupokea na kushughulikia maombi ya usajili kutoka kwa wataalamu wa mipangomiji wanaotembelea banda hilo.

Maafisa wa TPRB wanatoa huduma ana kwa ana kwa waombaji, ikiwa ni pamoja na kupokea nyaraka za usajili, kutoa maelekezo ya taratibu husika, na kusaidia kuhakikisha maombi yanawasilishwa kwa usahihi na kwa wakati.
Awali akizungumza katika maonesho hayo, Kaimu Msajili wa TPRB, TP. Martha Mkupasi, alisema kuwa ushiriki wa Bodi katika Sabasaba unalenga kuwafikia wadau wengi zaidi na kurahisisha huduma za usajili kwa vitendo.

Alisema kuwa Bodi inaendwlea kutoa elimu ya shughuli za mipangomiji kwa wananchi, ushauri pamoja na kupokea kero mbalimbali zinazohusiana na Bodi hiyo.
Katika muendelezo wa maonesho hayo, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe. Dkt. Leonard Akwilapo, alitembelea banda la TPRB na kuipongeza Bodi kwa juhudi zake za kuboresha huduma na kuwasogezea wananchi huduma muhimu.
Aidha, Waziri huyo amesisitiza umuhimu wa Bodi kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na kutoa huduma bora.

Pia, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bi. Lucy Kabyemela, alitembelea banda hilo na kujionea huduma zinazotolewa pamoja na kupongeza jitihada za Bodi katika kusogeza huduma karibu na wananchi.
TPRB inashiriki maonesho hayo, yaliyoanza rasmi Juni 28 na yanatarajiwa kuhitimishwa Julai 13, 2026 jijini Dar es Salaam.


