Na Winfrida Mtoi
MASHINDANO ya mchezo wa kuogelea ‘Taliss -IST Championship’ yameanza leo Februari 14, 2026. yakishirikisha jumla ya vilabu 17, kutoka ndani na nje ya Tanzania, ikiwamo pia watu wenye mahitaji maalumu.
Michuano hiyo ya siku mbili iliyoandaliwa na klabu ya kuogelea ya Taliss- IST, inafanyika kwenye bwawa la Shule ya Kimataifa Tanganyika(IST), Masaki jijini Dar es Salaam.
Akizungumzia mashindano hayo kocha wa klabu ya Taliss, Alex Mwaipasi amesema ni miaka 17 tangu wameanzisha michuano hiyo na mwaka huu umekuwa na utofauti mkubwa kwani ni mara ya kwanza wanahusisha watu wenye mahitaji maalumu.
“Kitu cha pekee kwenye mashindano haya ni kwamba tuna wenzetu wenye mahitaji maalumu, tumefanya hivi ili kuleta usawa kwenye michezo kwa sababu hawa vijana hawajazoea kuona wenzao wenye changamoto kwa kuwa ngazi ya kimataifa wanakuwa na michezo yao”
“Mwaka huu umekuwa wa mafanikio makubwa, tumefanikiwa kuleta jumla ya vilabu 17, viwili vinatokea Malawi, kimoja Rwanda na nyingine ni kutoka hapa nyumbani ikiwemo Zanzibar,” amesema Mwaipasi.
Kwa upande wake kocha anayefundisha watu wenye mahitaji maalumu, Anthony Josias, amesema wameomba kushiriki mashindano hayo kutokana na mara nyingi vijana hao kukosa nafasi ya kuwepo katika mashindano ya kuogelea.
“Leo nimekuja nao wawili lakini kwa ujumla kwenye timu wapo sita. Lengo ni kutaka kuonesha kuwa na wao ni sehemu ya jamii na kuondokana na dhana kuwa hawawezi,” ameeleza Anthony.


