Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Afya, Jenista Mhagama ameziagiza hospitali zote za umma nchini kutekeleza kwa ukamilifu maelekezo yaliyokwishatolewa na Serikali ya kupiga marufuku hospitali na vituo vya afya kuzuia maiti kwa kigezo cha kutolipwa gharama za matibabu.
Waziri Mhagama ametoa agizo hilo mkoani Tabora, wakati wa maadhimisho ya Wiki ya Chanjo Kitaifa na kuongeza kuwa wahudumu wa afya watakaoendelea kuzuia maiti kuzikwa watachukuliwa hatua za kisheria.

“Kumekuwa na kelele nyingi za upatikanaji wa maiti pale wenzetu wanapotangulia mbele za haki, ninawaomba vituo vyote vinavyotoa huduma za afya nchini maelekezo ya Serikali hayajabadilika, tunao waraka wa mwaka 2021 ambao umetoa maelekezo ya namna gani ya kushughulikia suala zima la huduma kwa maiti pale kifo kinapotokea.
“Ninawaagiza tena Waganga Wafawidhi wote rudini angalieni muongozo tulioutoa acheni kuleta usumbufu kwa wananchi wa Tanzania, hatutaendelea kumfumbia mtu macho ambaye hatozingatia waraka ambao wizara na Serikali uliutoa wa upatikanaji wa maiti pale wenzetu wanapotangulia mbele za haki,” amesema na kuongeza kuwa:

“Wakati mwingine inashangaza, aliyefariki huyo ndiye aliyekuwa na uwezo wa kujihudumia na kujilipia matibabu, waliobaki hawana uwezo, sasa unadai nini huyo marehemu sasa afufuke atoe hela ndio muweze kumuachia?, haiwezekani, naomba fuateni waraka wetu, maelekezo yako wazi, tunashangaa kituo cha afya wapo baadhi ya watu wakifariki mila au imani za dini zinawataka wazikwe haraka tunapochelewesha hiyo michakato tunawakosea haki,”.