Na Winfrida Mtoi, Mwanza
MKOA wa Mwanza umeweka bayana utayari wake wa kutoa maeneo ya uwekezaji kwa watu binafsi na Serikali kutokana na fursa nyingi zinazopatikana katika mkoa huo.
Hayo yameelezwa na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Chagu Nghoma alipomwakilisha Mkuu wa Mkoa wa huo, Said Mtanda katika Mdahalo wa Kitaifa uliondaliwa na Kituo cha Ubia wa Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPPC) wenye Mada Kuu ya ‘Ubia wa Sekta ya umma na Sekta Binafsi katika Muktadha wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 uliofanyika kwenye Ukumbi wa hoteli ya Gold Crest, jijini Mwanza.

Mhandisi Nghoma amesema kuna fursa nyingi ya uwekezaji za kukuza uchumi katika Mkoa huo, ikiwamo sekta ya Uchumi wa Buluu ukilenga ufugaji wa samaki na shughuli nyingine zinazofanyika katika Ziwa Victoria.
Amesema pamoja na hayo pia kuna maeneo mengi yanayofaa kwa ufugaji wa mifungo kama vile Ng’ombe na Mbuzi.
Ameeleza kuwa kuhusu uchumi wa Buluu kuna ufugaji wa samaki ambayo inahitaji kwa kiasi kikubwa uwekezaji wa viwanda na kuwekeza katika chakula cha samaki, pia viwanda vya nyama vinahitajika zaidi.

“Mkoa wa Mwanza una maeneo mengi ya uwekezaji na Mkoa upo tayari kuyatoa maeneo hayo kwa watu binafsi na Serikali. Uchumi wa mtu unaanza na mtu binafsi, ni lazima kufikiria nini unataka kufanya katika kuboresha uchumi binafsi na nchi,” amesema.