Na Mwandishi Wetu
MBUNGE wa Kisesa, Luhaga Mpina, hatakuwa miongoni mwa wanaowania ubunge kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) baada ya jina lake kukosa katika orodha ya watia nia waliopitishwa na Kamati Kuu ya chama hicho.
Taarifa hiyo imeelezwa leo, Jumanne Julai 29, 2025, na Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, Amos Makalla, alipoweka wazi majina ya walioteuliwa kuingia kwenye mchujo wa kura za maoni.
Katika Jimbo la Kisesa, Kamati Kuu imewateua watia nia saba ambao ni: Lusingi Makanda, Silinde Mhachile, Joel Mboyi, D. Madili Sakumi, Godfrey Mbuga, Elias Mambembela na Gambamala Michael Luchuga ambapo watapigiwa kura na wajumbe wa CCM Agosti 4, 2025 ili kumpata mgombea rasmi wa chama.

Mpina, ambaye ameliongoza jimbo hilo tangu mwaka 2005, alikuwa miongoni mwa wabunge wenye msimamo mkali na waliokuwa wakitoa kauli zenye ukosoaji dhidi ya baadhi ya maamuzi ya serikali.
Aliwahi kushika nyadhifa mbalimbali serikalini ikiwemo Naibu Waziri wa Muungano na Mazingira pamoja na Waziri wa Mifugo na Uvuvi kati ya mwaka 2017 hadi 2020.
Miongoni mwa matukio yaliyotikisa wakati wa ubunge wake ni pamoja na kumkosoa Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, kuhusu sakata la sukari, tuhuma ambazo baadaye zilibainika kukosa ushahidi na kusababisha Mpina kupewa adhabu ya kutohudhuria baadhi ya vikao vya Bunge.