Na Tatu Mohamed
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Albert Chalamila ametoa muda wa wiki moja kuanzia machi 2, 2026 kwa makundi ya watu wanaojihusisha na vitendo vya utapeli na unyang’anyi wa mali ikiwemo ardhi kujisalimisha kwa kurudisha mali walizozichukua kwa wamiliki halali kwani hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wote watakaokiuka agizo hilo.
Kauli hii imekuja kufuatia ziara ya Mkuu huyo wa Mkoa wa Dar es salaam aliyoifanya katika Wilaya ya Kinondoni na kubaini kukithiri kwa vitendo hivyo ambapo baadhi ya watu wamekuwa wakitumia njia ya kukodisha maeneo na baadae kufanya utapeli.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Machi 2, 2026 jijini Dar es Salaam, Chalamila amesema wamebaini uwepo wa kiwango kikubwa cha utapeli na unyang’anyi wa ardhi na kusababisha vilio kwa baadhi ya makundi ya watu ikiwemo wajane na warithi.
“Pia tumebaini uwepo wa utapeli kwenye show room za kuuzia magari ambapo watu wamekuwa wakilipia magari na kudhulumiwa kwa kisingizio kuwa magari yao bado yapo bandarini lakini pia Serikali imebaini uwepo wa mikopo isiyokuwa na tija inayowaumiza wananchi kupitia masharti magumu hivyo tunakwenda kuchukua hatua,” amesema Chalamila na kuongeza:

“Ninatoa muda wa wiki moja kuanzia leo Machi 2, 2026, wananchi wote ambao wana madai ya kutapeliwa ama kudhulimiwa mali zao ikiwemo ardhi kuwasilisha malalamiko yao kwenye ofisi yangu kwani nimekusudia kufanya ziara maalumu ya kufuatilia na kutatua migogoro hii kuanzia Machi 9 mwaka huu,”.
Aidha RC Chalamila ameipongeza Mahakama na TAKUKURU kwa namna wanavyoshugulikia kesi hizo huku akitoa tahadhari kwa baadhi ya wasimamizi wa mirathi wanaouza mali za warithi halali kwa kisingizio cha kulea ama kusomesha watoto wa marehemu.



