Na Mwandishi Wetu
Jeshi la Polisi mkoani Kagera linawashikilia watu wawili akiwamo mhudumu wa mochwari kwa tuhuma za kukutwa na viungo vinavyohisiwa kuwa ni vya binadamu katika nyumba moja ya wageni iliyopo Kata ya Kibeta Manispaa ya Bukoba, mkoani Kagera.
Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kagera, Blasius Chatanda, amesema watuhumiwa hao ni Piason Mdolo (42) anayejishughulisha na kazi za uganga wa kienyeji wilayani Mbozi Mkoani Songwe na Randan Mlomo (64) ambaye ni mtumishi wa chumba cha kuhifadhi maiti katika Hospitali ya Vwawa wilayani Mbozi, mkoani Songwe.
Kamanda Chatanda ametaja baadhi ya viungo walivyokutwa navyo watuhumiwa hao kuwa ni mfupa wa taya la binadamu, kipande cha moyo wa binadamu, kipande cha sehemu za siri za mwanamke, kondo la nyuma la tumbo la uzazi pamoja na ngozi za nyoka.
Amesema mdolo alikamatwa Juni 17,2025 akiwa na viungo hivyo na alipohojiwa, alidai kuwa alihitaji kuvitumia kwa matumizi yake binafsi na kumtaja Mlomo kuwa ndiye aliyempatia viungo hivyo.
Amesema Jeshi la Polisi mkoani Kagera linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo kabla ya kuwafikisha watuhumiwa hao katika vyombo vya sheria.
Aidha, ametoa onyo kali kwa watu wote wanaojihusisha na shughuli za uganga wa jadi bila kuwa na vibali halali, akisema hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ili kudhibiti vitendo vinavyohatarisha maisha ya watu na kukiuka sheria za nchi.


