Na Mwandishi Wetu
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Kamishna Msaidizi Richard Abwao, amesema mwanamke mmoja aliyefahamika kwa jina la Catherine Fito, mwenye umri wa miaka 21 mkazi wa Umanda Kata ya Kalunde Manispaa ya Tabora, amejiua kwa kunywa sumu ya kuulia wadudu, huku chanzo cha kifo hicho ikiwa ni wivu wa mapenzi.
Akithibisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda Abwao, amesema limetokea Juni 14,2025, ambapo mwanamke huyo anadaiwa kuwa katika mgogoro na mwenza wake kwa muda, hali iliyofanya kuchukua uamuzi huo.
“Tuna tukio moja la mwanamke kujiua kwa kunywa sumu ya kuulia wadudu huko katika kijiji cha Umanda, Kata ya Kalunde Manispaa ya Tabora, aliyetambulika kwa jina la Catherine Fito mwenye umri wa miaka 21, ilipofika saa nne usiku siku ya tarehe 14 Mume wa marehemu alifika nyumbani kwake na kumkuta mwanamke huyo anagalagala chini nje akiwa anatapika na alipumuuliza akajibu amekunywa sumu ya kuulia wadudu.
“Mgonjwa alipatiwa huduma ya kwanza katika zahanati ya Umanda na baada ya hapo akapewa Rufaa ya kwenda hospitali ya Milambo, lakini hawakufanya hivyo ndugu zake wakamchukua kumrudisha nyumbani na ilipofika saa kumi na mbili jioni siku ya tarehe 15 akafariki dunia akiwa nyumbani kwake na chanzo cha kifo hiki ni wivu wa kimapenzi.