Na Mwandishi Wetu
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, imekubali maombi ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu la kujitetea mwenyewe katika kesi ya uhaini inayomkabili na kuwaondoa mawakili wake 30 waliokuwa wakimtetea katika kesi hiyo.
Maombi hayo yaliwasilishwa na Lissu mwenyewe mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Franko Kiswaga ambaye alikubali ombi hilo, akieleza kuwa Lissu atakuwa huru kujibu hoja za upande wa mashtaka yeye binafsi hadi pale atakapoamua kuhitimisha utetezi wake.
Lissu ameeleza kuwa hana muda wa kuzungumza na mawakili wake akiwa gerezani na hataki wabebeshwe lawama kwa lolote litakalotokea.

Amesema kwa siku 68 alizokaa mahabusu imeshindikana kuzungumza na mawakili wake na akaona isiwe sababu ya wao kulaumiwa na kuonekana hawajamtetea ipasavyo.
Ameeleza kuwa katika siku hizo 68, wiki moja alikuwa gereza Keko na tangu Ijumaa Kuu alihamishiwa gereza la Ukonga lakini mawakili wake walikuwa hawaruhusiwi kuzungumza naye kwa faragha wala ruhusa ya kubadilishana nyaraka na wanazungumza kwa simu.
“Kama mfungwa mwenye mawakili, nina haki ya kuonana na mawakili kwa faragha na si mapenzi ya bwana jela,” amesema Lissu.
Lissu ameiambia Mahakama kuwa amekuwa akipitia mateso na ananyimwa haki ya kuabudu akiwa mahabusu na kusema kuwa hatua hiyo ni kinyume cha sheria na haki za binadamu na katiba ya nchi wakati wafungwa na mahabusu wengine wakipata haki hiyo.
Hata hivyo Mahakama imeahirisha kesi hiyo ya uhaini hadi Julai 1, 2025 kwa ajili ya kusubiri Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kupitia jalada la kesi hiyo ili kuona kama iende Mahakama Kuu au hapana.
Hatua hiyo inatokana na upande wa mashtaka kuomba ahirisho mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Kiswaga ambapo Wakili wa Serikali Mkuu, Nassoro Katuga alisema jalada la kesi hiyo lipo kwa DPP analipitia kisha atatoa taarifa kuhusu upelelezi ulipofikia na kama kesi hiyo iende Mahakama Kuu au hapana.
Lissu anadaiwa kutenda kosa hilo Aprili 3, 2025 ndani ya Jiji la Dar es Salaam kuwa siku hiyo kwa nia ya uchochezi aliushawishi umma kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, huku akitamka na kuandika maneno kumshinikiza kiongozi Mkuu wa Serikali ya Tanzania.
Juni 2, 2025, upande wa mashtaka ulieleza Mahakama kuwa jalada la upelelezi liliwasilishwa kwa DPP lakini baada ya kulipitia alibaini kuwepo kwa mapungufu yaliyohitaji kurekebishwa, hivyo kuwasilisha tena kwa wapelelezi.
Kutokana na hali hiyo, Wakili wa Serikali Nassoro Katuga aliomba mahakama kuahirisha kesi hiyo hadi tarehe nyingine ambapo Hakimu Kiswaga alikubali na kupanga kutajwa tena Julai 1,2025.