Na Mwandishi Wetu
BODI ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) leo tarehe 31 Mei 2025, imetembelea miundombinu ya gesi asilia iliyoshindiliwa (Compressed Natural Gas – CNG) iliyopo jijini Dar es Salaam, kwa lengo la kujielimisha kuhusu maendeleo ya sekta ndogo ya gesi asilia nchini.
Ziara hiyo imehusisha kutembelea vituo vya utoaji wa huduma za CNG vya Rafiki na Tembo Energies vilivyoko Tabata ToT, pamoja na kituo cha TAQA Dalbit kilichopo barabara ya Sam Nujoma.
Aidha, Bodi hiyo imetembelea pia ofisi za Kampuni ya Shields Engineering and Safety Solutions ya uthibitishaji wa miundombinu ya CNG (CNG Certifier Company) iliyopo eneo la Ubungo Maziwa.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Nishati ya Bodi ya Wakurugenzi, Mha. Ngosi Mwihava, amesema kuwa lengo la ziara hiyo ni kupata uelewa wa kina kuhusu shughuli za wadau mbalimbali katika sekta ya gesi asilia, ili kuwezesha udhibiti madhubuti unaozingatia changamoto zilizopo.
“Katika mnyororo wa thamani wa gesi asilia, hasa upande wa matumizi, kuna wadau wengi wanaojihusisha na shughuli mbalimbali. Baadhi ya shughuli hizo zinasimamiwa na EWURA. Ili tuweze kuzidhibiti kwa ufanisi, tunahitaji kuelewa kwa undani namna zinavyotekelezwa na changamoto zinazojitokeza, ili kuzitafutia suluhisho,” amesema Mwihava.

Hadi kufikia sasa, kuna jumla ya vituo tisa (9) vya CNG nchini, ambapo viwili kati ya hivyo vinatumika kwa matumizi binafsi katika Kiwanda cha Saruji cha Dangote.
Gesi asilia iliyoshindiliwa nchini inatumika zaidi kwa ajili ya kuendesha magari, viwanda, na kwa shughuli za kupikia, mfano ukiwa ni katika Hoteli ya Serena iliyopo jijini Dar es Salaam.

Aidha, idadi ya magari yanayotumia gesi asilia imefikia 15,000, na idadi hiyo inaendelea kuongezeka kadri miundombinu na uhamasishaji unavyoimarika.