Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa ameeleza msimamo wa Serikali ya Tanzania kuhusu mabadiliko ya sera za misaada ya Marekani chini ya utawala wa Rais Donald Trump, akisisitiza kuwa Tanzania lazima ijikite katika kujitegemea kiuchumi.
Akizungumza bungeni jijini Dodoma leo, Alhamisi Februari 6, 2025, Majaliwa amesema kuwa Marekani, kupitia Shirika lake la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), imesitisha baadhi ya misaada iliyokuwa ikitolewa kwa Tanzania na nchi nyingine zinazoendelea.
Amesema kuwa mabadiliko hayo ni sehemu ya sera mpya za mambo ya nje za Marekani, ambazo zinaweza kuwa na athari kwa baadhi ya sekta nchini.

“Ni kweli kwamba Serikali yetu inaheshimu sera za mambo ya nje na tunatekeleza mikataba kwa mujibu wa makubaliano na nchi husika. Hata hivyo, tumeanza kuona mabadiliko katika sera za baadhi ya nchi zenye uwezo mkubwa kama Marekani na haya mabadiliko yanaweza kuathiri baadhi ya nchi ikiwemo Tanzania,” amesema Majaliwa.
Pamoja na hilo, Majaliwa amesisitiza kuwa Tanzania imejipanga kuhakikisha kuwa uchumi wake unajitegemea ili kuepuka utegemezi wa misaada ya nje.