Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Kenya, William Ruto, anatarajiwa kuhutubia Bunge la Tanzania Mei 5, 2026, hotuba itakayofuatliwa na viongozi mbalimbali wa kitaifa.
Akisoma tangazo la Katibu wa Bunge leo Aprili 29, 2026 Bungeni jijini Dodoma, Naibu Spika wa Bunge, Daniel Sillo, amesema ujio wa Rais huyo unalenga kuimarisha ushirikiano wa kikanda, hususani katika nyanja za biashara, uwekezaji na maendeleo ya kiuchumi kati ya Tanzania na Kenya.
Ameeleza kuwa hotuba ya Rais Ruto inatarajiwa kuwa sehemu muhimu ya kikao hicho, huku akiwahimiza wabunge wote kuhudhuria bila kukosa.
“Tukio hili muhimu na la kihistoria ambalo pia litafuatiliwa na viongozi wakuu wa Kitaifa linalenga ushirikiano wa kindugu kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Jamhuri ya Kenya. Waheshimiwa wabunge wote mnahimizwa kuhudhuria bila kukosa siku hii muhimu ili kumsikiliza mgeni huyo wa Kitaifa akilihutubia Bunge na Taifa,” amesema Daniel Sillo


