Na Winfrida Mtoi
Tanzania imepata fursa ya kuandaa mkutano wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika ambao utaongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan akiwa ni Mwenyekiti kwenye ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, Dar es Salaam
Akizungumza na waandishi wa habari leo, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, January Makamba amesema mkutano huo utafanyika kwa siku mbili, Mei 24-25, 2024 ukihusisha viongozi mbalimbali wa Afrika.
Makamba amesema mkutano huo ni kumbukizi ya miaka 20 tangu kuanzishwa kwa baraza hilo, huku akiitaja Tanzania kuwa na historia ya kitovu cha harakati za ukombozi barani Afrika na mambo ya amani, ulinzi na usalama.
“ Nchi yetu ilitoa sapoti kubwa katika harakati za ukombozi hivyo Tanzania inaheshimika sana duniani na barani Afrika kwa mchango wake mkubwa wa ukombozi .
“Kama Tanzania hili jukumu ni heshima na wajibu, amani ndio moja ya chanzo cha sifa yetu kama nchi kuwa hatuko nyuma katika harakati za kutafuta amani na usalama barani Afrika kama ambayo hatukuwa nyuma wakati wa kutatuta uhuru na ukombozi wa bara la Afrika,”ameeleza.
Waziri huyo amesema kuwa katika baraza hilo kutakuwa na mazungumzo, majadiliano kuhusu hali ya ulinzi na usalama barani Afrika kwa miaka 20 iliyopita na muelekeo ujao.
Amewataja baadhi ya viongozi watakaodhuria mkutano huo kuwa ni Marais wa nchi za Gambia, Msumbiji, Uganda na Marais wengine wastaafu wa Afrika wakiongozwa na Dk. Jakaya Kikwete na Joaquim Chissano wa Msumbiji, Rais Mstaafu wa Nigeria ambao wamealikwa.