Serikali kuajiri wahudumu wa afya jamii 137,294

Na Esther Mnyika

Makamu wa Rais, Dk. Philip Mpango, amesema jumla ya wahudumu  wa afya 137,294 wa ngazi ya  jamii wataajiriwa  na kuwajengea uwezo  katika mikoa 26 ya Tanzania Bara.

Hayo ameyasema leo Januari 31,2024 wakati wa uzinduzi wa Mpango Jumuishi wa Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii uliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Amesema ni lazima kuweka mfumo mzuri wa uratibu wa shughuli za mpango huo na kuhakikisha taarifa za utekelezaji zinapatikana ikiwemo kutumia mifumo ya kidijitali.

“Katika kutekeleza mpango huu Serikali  imepanga  kutumia kiasi cha shilingi bilioni 899.473 kwa kipindi cha miaka mitano na
kiasi cha bilioni  99.678 ambazo zitahitajika katika mwaka wa kwanza wa utekelezaji kwani uwekezaji huu ni mkubwa sana ambao unahitaji rasilimali watu,” amesema Dk.Mpango.

Ameeleza kuwa mpango huo utafanyika katika kipindi cha miaka mitano kwa awamu ambapo katika mwaka wa kwanza (2023/24) zaidi ya wahudumu 28,000 watafikiwa na na  wahudumu 27,324 kila mwaka kwa kipindi cha miaka minne mfululizo kuanzia mwaka 2024/25 hadi 2027/28.

Amesema mpango huo ambao umezinduliwa leo ambapo wahudumu wa afya ngazi ya jamii watapata aina nne za mafunzo ambazo ni elimu ya afya, huduma za afya kinga huduma tembezi na mkoba na baadhi ya huduma  za tiba na kabla  ya kutoa vifaa  vya kutatua changamoto mbalimbali za afya nchini.

Amesema  mambo ambayo yapewe kipaumbele pamoja na lishe, afya ya mama, mtoto, vijana na uzazi wa mpango,  magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza, usafi wa mazingira, magonjwa ya mlipuko  na mabadiliko  ya  tabianchi.

Amesema utekelezaji wa  mpango huo unazingatia kanuni taratibu na miongozo iliyopo.

Dk. Mpango amewaelekeza viongozi wote wanaohusika katika ngazi zote kuhakikisha zoezi la kuwachagua wahudumu  hao linafanyika kwa kufuata vigezo na taratibu zilizowekwa ili waweze  kupata wahudumu  wenye sifa stahiki.

Pia amezisisitiza Wizara ya Afya,  Ofisi ya Rais _TAMISEMI  na Mamlaka zingine zinazohusika  kuhakikisha kuna usimamizi madhubuti wa mpango huo ili  kufikia malengo yake.

“Ni lazima kuweka mfumo mzuri wa kuratibu  shughuli za mradi  huu na taarifa za utekelezaji zinapatikana,” amesema.

Aidha amesema wanaweza kujifunza uzoefu kutoka visiwani Zanzibar  ambao wameanza kusimamia na kutekeleza  mradi huo kwa kutumia mifumo ya kidigitali tangu Desemba 16,2023.

Dk. Mpango ameitaka Wizara ya Afya  kutoa hamasa na elimu ya kutosha kwa jamii kuhusu mpango jumuishi wa wahudumu wa afya ngazi ya jamii  ili kurahisisha utekelezaji wake.

Dk. Mpango  ametoa rai kuwa masuala  ya lishe bora na usafi wa mazingira  yasiachwe nyuma katika kutekeleza mradi kama njia mojawapo  ya kujenga afya na kudhibiti  magonjwa ambayo yanatokana na uchafu.

Kwa upande wake Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, amesema mpango huo umelenga kupunguza idadi ya wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa kuimarisha huduma za afya kinga pamoja na kuongeza tija na ufanisi katika kutoa huduma za afya kufikia lengo la afya kwa wote.

Ameongeza kuwa  utasaidia pia kukabiliana na upungufu wa vituo vya afya  hususani katika maeneo ya vijijini.

“Kupitia mpango huu wahudumu wa afya ngazi ya jamii wameweza kuibua magonjwa mbalimbali yanayoikabili jamii kama vile Kifua Kikuu, Kipindupindu na ugonjwa wa Marburg,” amesema Ummy.

Amesema kupitia mpango huo wataweza kupunguza gharama za matibabu kutokana na kutambulika kwa ugonjwa katika hatua za awali zaidi.

Amesema umuhimu wa wahudumu hao ngazi ya jamii ni daraja kati ya vituo vya kutolea huduma na jamii husika kwa kuwa wamekuwa wakitambua mapema maradhi yanayojitokeza.

Ummy  amesema katika kuchagua wahudumu wa afya ngazi ya jamii suala la wakazi wa eneo husika litazingatiwa ili kuendana na mila na desturi za wananchi wa eneo hilo.

spot_img

Latest articles

Baraza la saba la Wafanyakazi Wizara ya Nishati lakutana Dodoma

📌 Dkt. Kazungu asema Wizara itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya Kimkakati 📌 Baraza lapitisha rasimu...

Wizara ya Nishati yataja mafanikio utekelezaji majukumu 2024/25

📌 Uzalishaji umeme waongezeka kwa asilimia 59.9 📌 Misheni 300 kuongeza upatikanaji umeme...

Gavana Tutuba: Hali ya uchumi wa Tanzania inaendelea kuimarika

Na Tatu Mohamed GAVANA wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba amesema kuwa, hali...

Dkt. Biteko: Ufundi Stadi umepewa kipaumbele na serikali

📌 Asisitiza kuwa, Rais Samia anajenga vyuo kila wilaya nchini 📌 Apongeza utoaji wa mafunzo...

More like this

Baraza la saba la Wafanyakazi Wizara ya Nishati lakutana Dodoma

📌 Dkt. Kazungu asema Wizara itaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya Kimkakati 📌 Baraza lapitisha rasimu...

Wizara ya Nishati yataja mafanikio utekelezaji majukumu 2024/25

📌 Uzalishaji umeme waongezeka kwa asilimia 59.9 📌 Misheni 300 kuongeza upatikanaji umeme...

Gavana Tutuba: Hali ya uchumi wa Tanzania inaendelea kuimarika

Na Tatu Mohamed GAVANA wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Emmanuel Tutuba amesema kuwa, hali...