Na Mwandishi Wetu, Iringa
KAMPUNI ya Media Brains kwa kushirikiana na Taasisi ya Konrad Adenauer Stiftung (KAS) imetoa mafunzo kwa waandishi wa habari mkoa wa Iringa kuhusu uandishi wa habari za kidijitali.
Mafunzo hayo ya siku mbili yaliyoeanza leo Juni 2, 2026, katika Hoteli ya Sunset, Manispaa ya Iringa, yanalenga kuwaongezea uwezo waandishi wa habari katika kuandaa, kuchakata na kusambaza habari kwa haraka huku wakizingatia misingi na maadili ya taaluma ya uandishi wa habari.



Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Ofisa Mtendaji Mkuu (CEO) wa Media Brain, Jesse Kwayu, amesema maendeleo ya sayansi na teknolojia pamoja na mabadiliko ya jamii, hususan vijana ambao wamejikita zaidi katika matumizi ya mitandao ya kijamii, yanawalazimu waandishi wa habari kuendana na mabadiliko hayo.
Ameeleza kuwa matumizi ya majukwaa ya kidijitali yanatoa fursa kwa waandishi wa habari kuwafikia watu wengi zaidi kwa wakati mfupi, hivyo ni muhimu kwao kuongeza ujuzi wa kutumia teknolojia hizo kwa ufanisi bila kuathiri ubora na uaminifu wa habari wanazozitoa.

“Wekezeni kwenye elimu, jifunzeni zaidi. Fanyeni uhakiki wa habari zenu, fanyeni ‘fact checking’ na zaidi, kuweni weledi. Fuateni maadili ya uandishi wa habari,” amesisitiza Kwayu.
Kwa upande wake Meneja Mradi kutoka Konrad Adenauer Stiftung, Damas Nderumaki, amesema ushirikiano wao na Media Brains ni kuhakikisha wanawanoa waandishi wa habari nchini kuhusu habari za kidigitali.
Katika mafunzo hayo washiriki watajifunza mbinu mbalimbali za uandishi wa habari za kidijitali, matumizi ya mitandao ya kijamii katika utoaji wa habari, pamoja na namna ya kukabiliana na changamoto zinazoibuka katika mazingira ya habari ya kisasa.





