Na Tatu Mohamed
BENKI ya CRDB imezindua rasmi msimu wa nne wa kipindi cha Zogo Mchongo, ikiendelea kutumia jukwaa hilo kutoa elimu ya fedha kwa Watanzania, kuhamasisha matumizi ya huduma za kifedha za kidijitali na kuwajengea wananchi uwezo wa kutambua na kutumia fursa za kiuchumi.
Uzinduzi huo uliofanyika jijini Dar es Salaam ulihudhuriwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda, ambaye alisema hatua ya benki hiyo kuendelea kuwekeza katika elimu ya fedha inaunga mkono juhudi za Serikali za kuongeza ujumuishi wa kifedha na kukuza uchumi wa wananchi.

“Nawapongeza CRDB kwa kuzindua msimu wa nne wa Zogo Mchongo. Hii si promosheni pekee, bali ni jukwaa la elimu linalowafikia wananchi walipo kupitia televisheni na mitandao ya kijamii, jambo linalosaidia kutekeleza maono ya Serikali na miongozo ya Benki Kuu kuhusu elimu ya fedha,” alisema Makonda.
Alisema Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi za fedha katika kuhakikisha elimu ya fedha inawafikia wananchi wengi zaidi ili kuwajengea uwezo wa kutumia fursa za kiuchumi zinazozalishwa nchini, ikiwemo matukio makubwa ya kimataifa yanayotarajiwa kufanyika Tanzania.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela, alisema msimu wa nne wa Zogo Mchongo unalenga kuendana na mabadiliko ya teknolojia na kuongeza uelewa wa wananchi kuhusu matumizi ya huduma za kifedha za kidijitali.
Alisema katika mazingira ya sasa ambapo huduma nyingi za benki zinapatikana kupitia mifumo ya kidijitali, elimu ya fedha imekuwa hitaji muhimu ili kuwawezesha wananchi kufanya maamuzi sahihi na kutumia huduma hizo kwa usalama na ufanisi.
“Tunataka elimu ya fedha isitolewe tena kupitia semina na mabango pekee, bali iwafikie wananchi kupitia maudhui wanayoyapenda kuyatazama kila siku. Ndiyo maana tumeendelea kuwekeza katika Zogo Mchongo kama jukwaa la kujifunza na kubadilisha mtazamo wa kifedha,” alisema Nsekela.

Aliongeza kuwa benki hiyo inaamini mteja mwenye maarifa ndiye mwenye uwezo wa kufanya maamuzi bora ya kifedha, hivyo kuimarisha ustawi wake na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa.
Nsekela alisema msimu huo pia utaangazia fursa zinazotokana na uchumi wa kidijitali, matumizi ya akili unde (Artificial Intelligence), pamoja na fursa zinazotokana na sekta za sanaa, michezo na ubunifu kuelekea matukio makubwa kama AFCON.

Aidha, alisema CRDB imeendelea kubuni bidhaa za kifedha zinazolenga makundi maalumu ikiwemo wakandarasi wa maudhui (content creators), wasanii na wabunifu, kwa kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu ili kuwawezesha kukuza biashara zao.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Masoko wa Benki ya CRDB, Joseline Kamuhanda alisema msimu mpya umeboreshwa kwa kuzingatia mabadiliko ya teknolojia na mahitaji ya wananchi, akibainisha kuwa lengo la benki ni kuhakikisha elimu ya fedha inawafikia Watanzania wengi zaidi kupitia burudani, maudhui ya kidijitali na majukwaa mbalimbali ya mawasiliano.

Kupitia msimu wa nne wa Zogo Mchongo, benki hiyo inalenga kuwafikia Watanzania wengi zaidi kwa maudhui yanayohamasisha ujasiriamali, uwekezaji, nidhamu ya fedha na matumizi sahihi ya huduma za kifedha, ikiwa ni sehemu ya mchango wake katika kufanikisha ajenda ya maendeleo ya uchumi wa Taifa.


