Johannesburg, Afrika Kusini
Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa ameafiki makubaliano kati ya Israel na Hamas kuhusu usitishaji wa mapigano kwa siku nne. Usitishaji wa mapigano utakuwa ndani ya saa 24.

Kama sehemu ya mpango huo, Hamas itawaachilia huru mateka 50 iliowakamata mwezi uliopita na Israel itawaachilia wafungwa wapatao 150 wa Kipalestina.
Katika taarifa yake, Ramaphosa ameema: “Kama mwanachama wa Jumuiya ya Kimataifa inayotetea amani, haki na utawala wa sheria za kimataifa katika sehemu zote za dunia, Afrika Kusini inaafiki makubaliano yaliyofikiwa.
“Ni matumaini yangu kwamba kufikiwa kwa usitishaji huu wa mapigano kutaimarisha juhudi za kufikia mwisho wa moja kwa moja wa mzozo uliopo,” amesema kiongozi huyo wa Afrika Kusini.
Ikumbukzwe kuwa, Serikali ya Afrika Kusini – inayoongozwa na African National Congress (ANC) – ni mshirika wa muda mrefu wa Wapalestina.
Aidha, imeitaka Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) kutoa hati ya kukamatwa kwa Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu ifikapo katikati ya mwezi Disemba kutokana na operesheni ya kijeshi ya Israel katika Gaza.
Ilianzisha operesheni kubwa ya kijeshi mjini Gaza kujibu shambulio la kuvuka mpaka la Hamas Oktoba 7, ambapo watu wasiopungua 1,200 waliuawa na wengine zaidi ya 200 kuchukuliwa mateka.
Wizara ya afya ya Gaza inayoendeshwa na Hamas imesema takriban watu 14,000 wameuawa katika eneo hilo tangu Israel ilipoanzisha kampeni yake ya kulipiza kisasi.