Na Winfrida Mtoi
Waandaaji wa pambano la Dar Boxing Derby wameweka gari aina ya Crown ikiwa ni zawadi kwa mshindi kati ya mabondia wa ngumi za kulipwa Tony Rashid na Juma Choki.
Pambano hilo kubwa linatarajiwa kufanyika Julai 24, 2026 jijini Dar es Salaam, huku kila bondia akitamani kuibuka mshindi ili kuondoka na gari hiyo.
“Mimi mwenyewe sina gari, nataka niwe mshindi ili nichukue hili. Nimejipanga vyovyote mpinzani wangu atakavyokuja ndiyo nitakavyocheza kwa kuwa makocha wangu wamemuangalia jinsi anavyocheza”, amesema Tonny Rashid leo Julai 17, 2026 wakati wakizungumza na waandishi wa habari.

Kwa upande wake Juma Choki amewaomba mashabiki kujitokeza kwa wingi kushudia burudani, kwani pambano lao limepewa thamani kubwa kutokana na zawadi iliyowekwa.
Naye Mratibu wa Matukio kampuni ya Peak Time ambao ni waandaaji wa pambano hilo, Bakari Hatibu amesema lengo la kutoa zawadi licha ya kuwalipa mabondia fedha, ni kuongeza thamani ya mchezo huo.
Sio mara ya kwanza kwa Peak Time kutoa zawadi ya gari kwa mabondia, waliwahi kufanya hivyo kwenye pambano la Dulla Mbabe na Twaha Kiduku ambapo mshindi alikuwa Kiduku.
Mabondia wengine watakaonogesha siku hiyo ni Dulla Mbabe akioneshana ubabe na Hussein Itaba, Haidary Mchanjo na Oscar Richard, wanawake ni Debora mwenda na Dorothea Mhoza, Sara Alex na Dorisia Mazige.


