Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuongoza mazishi ya Waziri Mkuu Mstaafu Hayati Edward Lowassa yanayotarajiwa kufanyika Wilayani Monduli Mkoani Arusha Jumamosi Februari17, 2024.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema leo (Jumapilii, Februari 11, 2024) kuwa, kabla ya mazishi hayo mwili wa Hayati Lowassa unatarajiwa kuagwa katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam na Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.
Akitoa taarifa ya ratiba ya mazishi ya kiongozi huyo katika Ofisi Ndogo ya Waziri Mkuu Oysterbay, Dar esSalaam, Majaliwa amesema Jumanne Februari 13, 2024 mwili wa Hayati Lowasa unataangwa na viongozi na wananchi katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam.
Jumatano Februari 14 mwili wa Hayari Lowasa utapelekwa katika Kanisa la KKKT Azania Front kwa ajili ya ibada takatifu na kuaga na Alhamisi Februari 15 mwili wa Hayati Lowassa utasafirishwa kwenda jijini Arusha ambako viongozi na wananchi watapa fursa ya kuaga katika viwanja vya Sheikh Amri Abeid.
Majaliwa amesema katika kipindi cha siku tano za maombolezo, Taifa litaendelea na shughuli za umma na kijamii sambamba na kushirikiana na wanafamilia katika ratiba ya msiba kama ilivyoandaliwa na kamati ya mazishi ya Kitaifa na wanafamilia.
Lowassa alifariki jana (Jumamosi, Februari 10, 2024) wakati akipatiwa matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) jijini Dar es Salaam na tangazo la kifo chake lilitolewa na Makamu wa Rais Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango.
Tayari Rais Samia alishatangaza siku tano za maombolezo ya kitaifa ambapo bendera zitapeperushwa nusu mlingoti kuanzia tarehe 10 Februari, 2024.


