Na Mwandishi Wetu
RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema kitaundwa chombo maalumu cha upelelezi kitakachoshughulikia masuala yaliyoainishwa katika ripoti ya Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, ikiwemo uchunguzi wa wahusika wa matukio ya uhalifu.
Rais Samia amesema chombo hicho kitafanya kazi ya kubaini watu waliohusika kupanga, kuratibu na kufadhili matukio hayo ya uvunjifu wa amani.
Amezungumza hayo leo Aprili 23, 2026, wakati akipokea ripoti ya Tume hiyo Ikulu jijini Dar es Salaam, akisema chombo hicho kitaangalia kwa undani pia masuala ya madai ya watoto kutumika katika matukio hayo na hoja zinazohusu kutopatikana kwa baadhi ya miili.

Ameongeza kuwa chombo hicho kitashughulikia pia madai ya watu waliodaiwa kutekwa na taarifa zao kutopatikana pamoja na walioathirika nje ya maeneo ya vurugu.
Aidha ameahidi kukamilisha suala la mabadiliko ya Katiba kama alivyoahidi katika kipindi cha pili cha awamu ya sita ya uongozi wake, akibainisha kuwa ni miongoni mwa vipaumbele vilivyoainishwa katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Amesisitiza kuwa Katiba mpya ni ajenda muhimu kwa Taifa, na kwamba mchakato huo utafanyika kwa kuzingatia maslahi ya Watanzania.
“Mabadiliko ya Katiba ni kipaumbele cha Serikali katika awamu hii ya sita, na tutaikamilisha kama tulivyoahidi,” amesema Rais Samia.
Ameongeza kuwa kutokana na ripoti hiyo, kumebainika kuwepo kwa changamoto mbalimbali zilizopelekea kutokea kwa ghasia katika kipindi hicho, na ameahidi kuzifanyia kazi kwa kina ili kuhakikisha zinapatiwa ufumbuzi na nchi inaendelea mbele kwa amani na utulivu.


