Na Mwandishi Wetu
Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa Matukio ya vurugu yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, Jaji Othman Chande, amebainisha kuwa chanzo cha ghasia hizo ni matokeo ya changamoto za muda mrefu ndani ya jamii zilizokosa ufumbuzi, ikiwemo ugumu wa maisha na madai ya Katiba mpya.
Akizungumza leo Aprili 23, 2026, wakati akikabidhi ripoti ya tume hiyo Ikulu jijini Dar es Salaam, Jaji Chande amesema ugumu wa maisha unachangiwa na ukosefu wa ajira kwa vijana, hali ngumu ya uchumi, pamoja na mazingira yasiyo rafiki ya biashara yanayotokana na kodi na tozo nyingi.
Katika vyanzo vikuu vitano alivyovitaja, Jaji Chande amebainisha mambo ya siasa yakihusisha madai ya Katiba mpya, uimarishaji wa demokrasia ya vyama vingina shinikizo la uboreshaji wa Tume ya Uchaguzi, migogoro na malalamiko ya ndani ya vyama vya siasa.
Vyanzo vingine vilivyotajwa ni utendaji usioridhisha wa baadhi ya watumishi wa umma, hususani wa ngazi za chini, wanaotuhumiwa kutovishughulikia kero za wananchi, pamoja na mmomonyoko wa maadili katika jamii.
Vilevile, Jaji Chande amegusia nyanja ya mahusiano ya kimataifa, akisema baadhi ya mataifa hutanguliza maslahi yao binafsi, jambo linaloweza kuathiri utulivu wa nchi zinazoendelea kwa kutaka kunufaika na rasilimali zilizopo.
“Tume imebaini jumla ya maeneo 31 yaliyotajwa na mashahidi kama vitovu vya ghasia. Baada ya kuchakata orodha hiyo, tumetenga vyanzo vikuu vitano na vichocheo nane vilivyosababisha vurugu hizo,” amesema Jaji Chande.
Aidha, amevitaja vichocheo vya ghasia hizo kuwa ni kauli mbiu zilizovuma kipindi hicho kama vile “No reforms, no election”, “Samia must go”, na “Oktoba tunatiki”. Amesema kauli hizo zilitumiwa na baadhi ya wanasiasa, wakiwemo walioenguliwa kwenye mchakato wa uteuzi ndani ya vyama vyao, ili kuchochea vurugu kwa maslahi ya chini kwa chini.
Katika hatua nyingine, ripoti hiyo imesisitiza umuhimu wa maridhiano kama hatua ya kuponya majeraha na kurejesha umoja wa kitaifa.
“Kuna umuhimu wa kufanya majadiliano baina ya dini kama sehemu ya mchakato wa maridhiano ya kijamii. Hii itasaidia kuleta maelewano miongoni mwa viongozi wa dini na kuweka mipaka iliyo wazi kati ya shughuli za dini na siasa,” ameeleza Jaji Chande.


