Na Winfrida Mtoi
UONGOZI wa Klabu ya Simba umeweka wazi hatua kali za kinidhamu zilizochukuliwa dhidi ya mshambuliaji wao, Jonathan Sowah, ikiwemo kuondolewa kwenye kikosi cha wakubwa na kutakiwa kufanya mazoezi na timu ya vijana (U-20).
Hatua hiyo imekuja kufuatia malalamiko mfululizo kutoka kwa Benchi la Ufundi la klabu hiyo, yaliyomtuhumu mchezaji huyo kwa makosa mbalimbali ya utovu wa nidhamu.
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba, Ahmed Ally, amefafanua leo Aprili 14, 2026, kuwa sakata hilo lilianza kushika kasi mwezi Machi wakati timu hiyo ilipokuwa safarini jijini Dodoma.
”Mwezi wa tatu tulipokuwa Dodoma kwa ajili ya mchezo dhidi ya Dodoma Jiji, Sowah aliamrishwa kuondoka kambini na kurejea Dar es Salaam mara moja kutokana na tuhuma za utovu wa nidhamu zilizowasilishwa na benchi la ufundi.
“Baada ya kurejeshwa Dar es Salaam, Sowah alifikishwa mbele ya Kamati ya Nidhamu ya klabu ambapo alisomewa mashtaka yake na mchezaji huyo alikiri baadhi ya makosa na kutoa maelezo kwa mengine.
Amesema kamati ilijiridhisha na makosa yake na kutoa adhabu mbili ya kulipa faini na kufanya mazoezi na timu ya vijana (U-20).
Uongozi umesisitiza kuwa adhabu ya kumshusha Sowah kwenye timu ya vijana si ya kudumu, bali ni kipindi cha mpito cha kumfanyia tathmini.
”Adhabu ya kufanya mazoezi na vijana inalenga kumpa nafasi ya kujitathmini na kuonyesha mabadiliko. Tukijiridhisha kuwa amebadilika, basi atarejeshwa kwenye kikosi cha wakubwa kuendelea na majukumu yake,” alihitimisha Meneja huyo.


