Na Mwandishi Wetu
Klabu ya Simba imepigwa faini ya Dola za Marekani 50,000 ( zaidi ya Sh. 100 milioni) na kuamriwa kucheza bila mashabiki katika mchezo wao ujao wa Ligi ya Mabingwa Afrika (CAF Champions League) dhidi ya Gaborone United ya Botswana, utakaopigwa kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Uamuzi huo umetolewa na Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF) baada ya Simba kukutwa na makosa ya mashabiki wake kufanya vurugu na kuwasha fataki kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho msimu uliopita dhidi ya Al Masry ya Misri, uliopigwa katika uwanja huo huo.Katika mchezo huo uliofanyika Aprili 9, 2025 kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam, Simba ilishinda kwa penalti 4-1 na kufuzu nusu fainali ya michuano hiyo kufuatia matokeo ya jumla kuwa sare ya 2-2.