Na Tatu Mohamed
MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Faustina Mfinanga (Nandy), amesema elimu aliyoipata katika Maonesho ya 49 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (Sabasaba) imefungua macho yake kuhusu umuhimu wa kutumia nembo ya Made in Tanzania katika shughuli zake za biashara na ubunifu.
Nandy, ambaye pia ni mjasiriamali anayejihusisha na biashara ya urembo, amesema awali alikuwa anaamini bidhaa bora lazima zitoke nje ya nchi, lakini sasa amehamasika kuzalisha ndani ya nchi baada ya kufahamu nguvu ya nembo ya Made in Tanzania.

“Nimepata elimu kubwa sana, kumbe naweza kuzalisha bidhaa zangu hapa hapa nchini na bado zikawa na hadhi ya kimataifa kwa kutumia nembo ya Made in Tanzania. Hili limenifungua macho na kunipa motisha mpya,” amesema Nandy wakati alipotembelea Banda la Made in Tanzania.
Amesema anatambua nafasi yake kama msanii mwenye ushawishi mkubwa, hivyo atatumia jukwaa hilo kuelimisha na kuhamasisha vijana wengine kuhusu uzalendo wa kutumia bidhaa za ndani zenye ubora.
Nembo ya Made in Tanzania, inayosimamiwa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade), inalenga kukuza utambulisho wa bidhaa za Kitanzania kwenye masoko ya ndani na ya kimataifa.

Kwa upande wake, Nandy ameahidi kuendelea kushiriki katika mafunzo mbalimbali ili kuwa balozi bora wa kuitangaza nembo hiyo duniani kupitia kazi zake za sanaa na bidhaa zake za kibiashara.