Na Mwandishi Wetu
Kamati ya Uchaguzi ya TFF imewang’oa wagombea watano wa nafasi ya Urais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na kubaki mmoja ambaye ni Wallace Karia anayetetea kiti hicho.
Akitangaza ripoti ya usahili wa uchaguzi huo Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa TFF, Wakili Kiomoni Kibamba, amesema Karia ndiye mgombea pekee aliyekidhi vigezo na kwa mujibu wa Kanuni na kama kuna mtu anapingamizi bado ana nafasi ya kufanya hivyo.
“Kwenye nafasi ya urais kulikuwa na wagombea sita, mmoja hakutokea kwenye usahili na wengine wanne hawakukidhi matakwa ya kikanuni, mgombea mmoja amekidhi matakwa yote ya kikanuni na tumempitisha ambaye ni Wallace Karia,”amesema Kibamba.
Kibamba ameeleza kuwa kwenye nafasi ya wagombea wa nafasi ya ujumbe kulikuwa na wagombea 19 ambapo 17 walihudhuria usahili, saba wamekosa vigezo na kumi wamepitishwa kuendelea na mchakato wa uchaguzi katika hatua inayofuata.
