Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) imetoa ufafanuzi kuhusu changamoto ya ukosefu wa huduma ya maji iliyowakumba wakazi wa maeneo yanayohudumiwa na Mtambo wa Uzalishaji Maji wa Ruvu Juu kuwa ni matengenezo makubwa yaliyolenga kuboresha na kuimarisha huduma zaidi.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano DAWASA, Bi. Everlasting Lyaro, amesema kukosekana kwa huduma hiyo tangu Machi 26,2026 kulitokana na utekelezaji wa kazi muhimu tatu katika mtambo huo, hatua inayolenga kuongeza ufanisi wa uzalishaji na usambazaji wa maji kwa wananchi.
Bi. Lyaro amesema kazi zilizofanyika na zilizosababisha kuzimwa kwa Mtambo wa Ruvu Juu ni pamoja na ukarabati wa bomba kubwa la inchi 48 linalosafirisha maji ghafi kutoka chanzo cha Mto Ruvu kwenda mtamboni, Usafishaji wa mabeseni ya kuchuja tope sambamba na zoezi la kufunga pampu mpya tatu.
“Tayari kazi ya kudhibiti uvujaji wa maji katika bomba la inchi 48 imekamilika, na tunatarajia huduma ya maji kwa wananchi wanaohudumiwa na mtambo huu kuanza kurejea taratibu kuanzia usiku wa leo Machi 27 kwa sehemu kubwa.
“Mamlaka inaomba radhi kwa changamoto iliyojitokeza,” amesema Bi. Lyaro.
Aidha, DAWASA imeeleza kuwa katika kuimarisha uhakika wa huduma ya Maji tayari Pampu nne za Maji zimewasili kati ya Pampu nane ambapo pampu tatu zimeanza kufungwa katika Mtambo wa Ruvu Juu na pampu moja katika Mtambo wa Ruvu Chini uliopo Wilaya ya Bagamoyo.
Lyaro amebainisha kuwa ujio wa Pampu hizi ni ishara ya nia thabiti ya Serikali ya awamu ya Sita ya kuboresha na kuimarisha upatikanaji wa Maji kwa Wananchi wake ndani ya eneo la kihuduma la DAWASA


