Na Mwandishi wa OTR
MSAJILI wa Hazina, Bw. Nehemiah Mchechu, ametaka kufanyika kwa mageuzi makubwa katika Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) ili kujenga taasisi yenye ufanisi zaidi, kuongeza tija na mapato, na kuimarisha ushindani wake katika soko la kisasa la habari na utangazaji.
Wito huo ulitolewa kwa Mkurugenzi Mkuu mpya wa TBC, Bi. Asha Dachi, Ijumaa, Agosti 28, 2026, jijini Dar es Salaam, alipotembelea Ofisi ya Msajili wa Hazina (OTR) kujadili mikakati ya kuipeleka TBC mbele zaidi.

Bw. Mchechu alisema kuwa, kama sehemu ya utekelezaji wa Dira 2050, anatamani kuona ndani ya miaka 10 ijayo TBC ikiwa chombo cha habari kinachoongoza kwa ubora, ubunifu na kuvutia hadhira.
“Mnapaswa kutatua changamoto ambazo ni kikwazo katika kutimiza mahitaji ya wateja wetu,” alisema Bw. Mchechu, ambaye katika mkutano huo aliambatana na wataalamu kutoka Idara ya Usimamizi wa Utendaji wa Mashirika ya Kibiashara pamoja na msaidizi wake.

“Mnapaswa kuhakikisha kuwa TBC inatoa huduma zinazokidhi mahitaji ya wananchi, huku ikitumia fursa zilizopo kujenga taasisi yenye ushindani na endelevu,” alisema.
Alisema kufanikisha mageuzi hayo kunahitaji timu imara ya kitaalamu itakayomsaidia Mkurugenzi Mkuu katika kutekeleza majukumu yake na kusukuma mbele agenda ya mabadiliko ya shirika.
Kwa upande wake, Bi. Dachi alimhakikishia Msajili wa Hazina kuwa TBC imejidhatiti kufanya mageuzi ya kiteknolojia yatakayoongeza tija na kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi.
“Mageuzi ya kiteknolojia ndiyo mstakabali wa TBC,” alisema Bi. Dachi, aliyeambatana na wataalamu wa sheria, mipango na uwekezaji, ukaguzi wa ndani, uhasibu na ufundi.


