Na Mwandishi Wetu
TAASISI ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imeongeza kasi ya tafiti za kijiosayansi nchini kwa lengo la kuvutia uwekezaji katika sekta ya madini, kuongeza ajira, mapato ya Serikali na kuimarisha mchango wa sekta hiyo katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
Akizungumza katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima ‘Nanenane’ yanayoendelea jijini Dodoma, Mkurugenzi Mtendaji wa GST, Eng. Ally Samaje, alisema taasisi hiyo ndiyo msingi wa maendeleo ya sekta ya madini kwa kuwa hukusanya, kuchakata, kuhifadhi na kusambaza taarifa muhimu za kijiosayansi zinazowawezesha wawekezaji kufanya maamuzi sahihi.
“Taarifa za kijiosayansi ndizo msingi wa uwekezaji katika sekta ya madini. Kadiri tunavyopanua utafiti, ndivyo tunavyopunguza hatari kwa wawekezaji, kuongeza uwezekano wa kufunguliwa migodi mipya na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika uchumi wa taifa,” alisema.

Alisema hadi sasa GST imekamilisha utafiti wa jiolojia katika asilimia 98 ya eneo la Tanzania, huku utafiti wa kijiofisikia wa kiwango cha kawaida ukifikia asilimia 100, hatua inayowawezesha wawekezaji kupata taarifa za awali kuhusu maeneo yenye rasilimali za madini.
Kwa upande wa utafiti wa kijiofisikia wa kina (High Resolution Airborne Geophysical Survey), alisema umefikia asilimia 16 ya eneo la nchi, lakini maandalizi ya kuongeza kiwango hicho yanaendelea kupitia programu mpya za urushaji ndege katika maeneo yenye fursa kubwa za madini.
“Awamu ya kwanza ya programu mpya itafanyika katika eneo linalokadiriwa kuwa asilimia 18 ya ukubwa wa Tanzania. Hii itatuwezesha kufikisha kiwango cha utafiti wa kijiofisikia wa kina hadi asilimia 34 mara baada ya kukamilika kwa kazi hiyo,” alisema.
Aliongeza kuwa awamu inayofuata itahusisha eneo la katikati mwa Tanzania lenye ukubwa wa takribani asilimia 19 ya nchi, hatua itakayowezesha taifa kufikia zaidi ya asilimia 50 ya utafiti wa kijiofisikia wa kina kabla ya mwaka 2030.
Alisema GST pia inaendelea kupanua utafiti wa kijiokemia, ambapo hadi sasa umefikia asilimia 24 ya eneo la nchi, huku maeneo 18 mapya yakitarajiwa kufanyiwa utafiti katika mwaka huu wa fedha ili kufikisha kiwango hicho hadi asilimia 30.
Aliongeza kuwa, maeneo mengi yaliyochaguliwa yana shughuli nyingi za uchimbaji mdogo, hivyo taarifa zitakazokusanywa zitawasaidia wachimbaji kufanya uchimbaji kwa uhakika badala ya kubahatisha.
“Tunataka kuwapa wachimbaji wadogo taarifa sahihi zitakazowawezesha kuongeza uzalishaji, kuboresha kipato na hata kupata mikopo kutoka taasisi za fedha kwa kutumia matokeo ya tafiti zetu kama msingi wa kujenga imani kwa wakopeshaji,” alisema.
Alibainisha kuwa utekelezaji wa tafiti hizo unawezeshwa na Mfuko wa Utafiti wa Madini unaofadhiliwa kupitia fedha za retention zinazotokana na shughuli za sekta ya madini.
Alifafanua kuwa, kongezeka kwa taarifa sahihi za kijiosayansi kutavutia wawekezaji zaidi, kuongeza shughuli za utafiti na uchimbaji, kuchochea uanzishaji wa migodi mipya, kuimarisha viwanda vinavyotumia madini kama malighafi na kuongeza mchango wa sekta ya madini katika ukuaji wa uchumi wa taifa kuelekea Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.


