Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) Wilaya ya Ubungo imeanza utekelezaji wa mpango wa kuboresha huduma ya maji katika Mtaa wa Kimara B kwa kulaza bomba lenye uwezo mkubwa zaidi, hatua inayolenga kukidhi mahitaji ya sasa ya wakazi na kuondoa changamoto ya upatikanaji wa maji iliyodumu kwa muda mrefu.
Akizungumza Agosti 6, 2026, wakati wa zoezi la kutembelea wateja, kukagua na kusoma mita za maji pamoja na kufuatilia hali ya upatikanaji wa huduma katika eneo hilo, Meneja wa Mkoa wa kihuduma DAWASA Ubungo, Mhandisi Anthony Budaga, alisema zoezi hilo ni sehemu ya mkakati wa Mamlaka wa kubaini changamoto zinazowakabili wateja na kuzitafutia ufumbuzi wa kudumu.

Alieleza kuwa ukaguzi huo unalenga kubaini mita zenye matumizi sifuri au matumizi madogo yasiyoendana na hali halisi, pamoja na kutathmini upatikanaji wa huduma ya maji nyumba kwa nyumba ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa wakati.
“Kimara B imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya upatikanaji wa maji kwa muda mrefu kutokana na ongezeko la idadi ya wakazi, huku miundombinu iliyopo ikiwa ilisanifiwa kuhudumia idadi ndogo ya watu. DAWASA imeandaa mpango wa kulaza bomba lenye uwezo mkubwa zaidi litakaloendana na mahitaji ya sasa na kuboresha upatikanaji wa huduma kwa wananchi,” amesema Mhandisi Budaga.

Aidha, amesema mradi huo utaongeza uwezo wa usambazaji wa maji, kuimarisha mtiririko wa huduma na kuhakikisha wananchi wa Kimara B wanapata huduma ya maji kwa uhakika.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Kimara B, Ndugu Beruki Kikwala, ameipongeza DAWASA kwa kufika eneo hilo na kufanya ukaguzi wa nyumba kwa nyumba, akisema hatua hiyo inaonesha dhamira ya Mamlaka katika kusikiliza na kutatua changamoto za wananchi.

“Leo tupo pamoja na DAWASA tukikagua mita na kuangalia hali ya upatikanaji wa maji katika kila nyumba. Lengo ni kubaini sababu zinazowafanya baadhi ya wananchi wapate maji na wengine wasipate, ili changamoto hii ipatiwe ufumbuzi wa kudumu,” amesema Kikwala.
Naye mkazi wa Kimara B, Ndugu Cesilia Masangula, amesema wananchi wa eneo hilo wamepokea kwa matumaini makubwa hatua zilizochukuliwa na DAWASA, akieleza kuwa changamoto ya maji imekuwa ikiathiri maisha ya kila siku, hususan wanawake na watoto ambao hulazimika kutumia muda mwingi kutafuta maji.
Amesema utekelezaji wa mradi wa kuboresha miundombinu ya maji pamoja na ukaguzi wa mita utasaidia kuongeza upatikanaji wa huduma na kuboresha ustawi wa wananchi wa Kimara B.


