Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SHIRIKA la Mawasiliano Tanzania (TTCL), kupitia Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Taarifa Kidijitali (National Internet Data Centre – NIDC), linatumia Maonesho ya Kitaifa ya Kilimo ya Nanenane yanayoendelea jijini Dodoma kuhamasisha wananchi, wanafunzi, taasisi na wafanyabiashara kutumia huduma za Cloud kuhifadhi taarifa na mifumo yao kwa usalama ndani ya Tanzania.
Akizungumza katika maonesho hayo, Mtaalamu wa TEHAMA wa TTCL Data Centre, Alfred Thawe, amesema huduma hiyo inalenga kutoa suluhisho salama na la gharama nafuu kwa watumiaji wanaohitaji kuhifadhi taarifa, kuendesha mifumo ya kidijitali na kupata huduma nyingine za TEHAMA bila kutegemea miundombinu iliyopo nje ya nchi.

Amesema kupitia huduma za Cloud, watumiaji wanaweza kuhifadhi taarifa zao (Storage as a Service), kuendesha mifumo mbalimbali (Infrastructure as a Service), pamoja na kusajili vikoa na kupata huduma nyingine za kidijitali kupitia miundombinu ya NIDC.
Thawe ameeleza kuwa moja ya faida kubwa ya huduma hiyo ni kwamba taarifa zote huhifadhiwa ndani ya Tanzania, jambo linaloongeza usalama wa taarifa, kulinda faragha za watumiaji na kuimarisha uhuru wa kidijitali wa taifa.
Ameongeza kuwa Kituo cha Taifa cha Kuhifadhi Taarifa Kidijitali kimefikia kiwango cha kimataifa cha Tier III, kinachoonyesha ubora wa miundombinu yake katika utoaji wa huduma za uhifadhi wa taarifa.

Aidha, amesema huduma hiyo inapatikana kwa wananchi wote, wakiwemo taasisi, kampuni, wanafunzi na wajasiriamali, ambapo kinachohitajika ni kujisajili kupitia mfumo wa NIDC kwa kutumia taarifa binafsi kama jina na barua pepe.
Thawe amewahimiza wananchi wanaotembelea Maonesho ya Nanenane kufika katika banda la TTCL ili kupata elimu kuhusu huduma za Cloud na kujifunza namna zinavyoweza kusaidia kuhifadhi taarifa na kuboresha uendeshaji wa shughuli zao za kila siku.


