Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SERIKALI kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji (NIRC) imezindua mkakati wa kutekeleza zaidi ya miradi 30 mipya ya umwagiliaji katika mwaka wa fedha 2026/27, huku ikitarajia kuajiri kati ya vijana 2,000 na 4,000 kupitia mpango wa uchimbaji wa visima na usimamizi wa miundombinu ya umwagiliaji.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima ‘Nanenane’ yanayoendelea jijini Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa NIRC, Raymond Mndolwa, amesema miradi hiyo inalenga kuongeza uzalishaji wa kilimo kwa kuhakikisha wakulima wanapata maji ya uhakika badala ya kutegemea mvua.

Amesema katika kipindi cha utekelezaji wa majukumu ya Tume hiyo, tayari wakandarasi 146 wanaendelea na ujenzi wa miradi mbalimbali ya umwagiliaji, huku miradi mingine 634 ikiwa katika hatua za usanifu.
“NIRC pia inatarajia kuanza rasmi ugawaji wa pampu za maji katika mikoa saba kuanzia Agosti 11 mwaka huu, ambapo zoezi litazinduliwa mkoani Katavi,” amesema
Amefafanua kuwa jumla ya pampu 1,000 za kawaida (surface pumps) zitatolewa kwa wakulima wa mbogamboga na matunda ili kuwawezesha kuvuta maji kutoka kwenye mito na mabonde kwa urahisi, huku zaidi ya pampu 1,000 zinazotumia nishati ya jua (solar pumps) zikitengwa kwa wakulima wa zao la parachichi.
Ameeleza kuwa, Tume imeandaa mpango wa kuunda vikundi vya vijana wenye ujuzi wa ufundi na uhandisi katika halmashauri zote 184 nchini ili washiriki katika uchimbaji wa visima, usimamizi wa miradi na ufungaji wa miundombinu ya umwagiliaji.
Amebainisha kuwa hadi sasa visima 415 tayari vimechimbwa, huku lengo la Tume likiwa ni kufikia visima 67,000 ndani ya kipindi cha miaka minane ijayo ili kuongeza eneo la kilimo cha umwagiliaji na kuimarisha usalama wa chakula nchini.
Aidha, amesema utekelezaji wa miradi hiyo unaunga mkono jitihada za Serikali za kuifanya sekta ya kilimo kuwa mhimili wa ukuaji wa uchumi kwa kuongeza tija, uzalishaji na kipato cha wakulima.


