Na Tatu Mohamed
KAMPUNI ya GASCO, kampuni tanzu ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), imesema itaendelea kuboresha huduma zake ili kuhakikisha miundombinu ya gesi asilia nchini inakuwa salama, yenye kuaminika na kuchangia maendeleo ya sekta ya nishati pamoja na uchumi wa Taifa.
Akizungumza katika Maonesho ya 50 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam (DITF) maarufu Sabasaba, Mhandisi Mitambo wa GASCO, Daud Enock, amesema pamoja na kufanya matengenezo ya miundombinu iliyopo, kampuni hiyo pia inashiriki katika ujenzi wa miundombinu mipya ya kusambaza gesi pale miradi mipya inapopatikana.
“Katika mwaka wa fedha uliopita, GASCO ilitekeleza miradi sita ya ujenzi wa miundombinu ya gesi katika maeneo mbalimbali ya Dar es Salaam, ikiwemo kuwaunganishia huduma ya gesi wateja wapya wa viwandani na kibiashara,”amesema.

Amesema GASCO inasimamia, inaendesha na kufanya matengenezo ya miundombinu yote ya gesi asilia inayomilikiwa na TPDC, ikiwemo mitambo ya kuchakata gesi ya Songosongo mkoani Lindi yenye uwezo wa kuchakata futi za ujazo milioni 140 kwa siku na mtambo wa Mtwara wenye uwezo wa kuchakata futi za ujazo milioni 210 kwa siku.
Amefafanua kuwa baada ya gesi asilia kuchakatwa na kusafishwa, husafirishwa kupitia bomba la gesi hadi Kinyerezi, Dar es Salaam, ambako husambazwa kwa matumizi ya uzalishaji wa umeme, viwanda, taasisi na matumizi ya majumbani.
“Miongoni mwa watumiaji wakubwa wa gesi hiyo ni viwanda, mitambo ya kuzalisha umeme, taasisi za umma pamoja na hoteli na majengo makubwa ya biashara,” amesema.
Enock amebainisha kuwa juhudi hizo ni sehemu ya mkakati wa kampuni wa kuhakikisha miundombinu ya gesi asilia nchini inafanya kazi kwa ufanisi kupitia matengenezo, ukarabati na ujenzi wa miundombinu mipya ili huduma ya gesi iwafikie watumiaji kwa uhakika.


