Na Winfrida Mtoi
TANZANIA imethibishwa rasmi kuwa mwenyeji wa mashindano makubwa la urembo duniani ‘Miss World 2027’, huku Serikali ikisema imejipanga kuhakikisha linafanyika kwa mtindo wa pekee wa kuvutia ili kuandika historia duniani.
Mkataba wa kuwa mwenyeji wa mashindano hayo la 74, umesainiwa leo Aprili 20, 2026, jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa, mbele ya Waziri wa wizara hiyo, Paul Makonda, ambapo Tanzania itakuwa nchi ya pili Afrika kuandaa ya kwanza ilikuwa Afrika Kusini.
Hafla ya kusaini mkataba huo, imehudhuriwa na warembo mbalimbali akiongozwa na Miss World 2025, Opal Suchata, Miss World Africa 2025, Hasset Dereje, pamoja na Miss World Tanzania 2026, Latricia Ian, aliyepata taji hilo jana jijini Dar es Salaam.


Wengine ni wadau wadau wa sekta ya urembo nchini akiwamo mwaandaaji wa shindano Miss World Tanzania, Mustafa Hassanali, wanamitindo maarufu wa kimataifa wa Tanzania Millen Magessa ambaye ni Miss Tanzania 2001, Miriamu Odemba aliyewahi kuiwakilisha nchi katika mashindano ya Miss Earth 2008 na Jokate Mwegelo mshindi wa pili Miss Tanzania 2006.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Makonda amesema jukwaa la Miss World linafuatiliwa na zaidi ya nchi 130, Tanzania ikitarajia kupata wageni wasiopungua 20,000. hivyo ili kulifanya kuwa bora zaidi Serikali itahusisha wadau mbalimbali katika maandalizi.
Ameeleza kuwa sherehe za mashindano hayo zitafanyika kwa siku 28, zikihusisha shughuli tofauti tofauti kama vile ufunguzi, chakula cha wageni, mashindano ya vipaji, chakula cha hisani, maonesho ya mitindo pamoja na fainali kubwa ya Miss World.


“Kwa hiyo mwakani tuna mwezi mzima wa warembo. Tanzania ipo tayari kupokea wageni kutoka mataifa mbalimbali kwa kuwa matukio yatakayofanyika katika kipindi hicho yatafungua fursa zaidi za kiuchumi,” amesema Makonda.
Aidha ameeleza kuwa mpango wa Serikali ni kuendelea kuomba kufanya mashindano ya Miss World kwa kipindi chote cha Uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ikilenga kuitangaza Tanzania kimataifa na kukuza Sekta za Utalii, Sanaa na Michezo.

Kwa upande wake Mwenyekiti na Mtendaji Mkuu wa Miss World, Julia Morley, aliitaja Tanzania kuwa ni sehemu yenye uzuri wa kipekee ambao bado haujajulikana kikamilifu duniani, akiahidi kusaidia ijulikane.
Julia ametoa wito wa ushirikiano wa karibu kati ya wadau wa habari na serikali katika kuitangaza Tanzania kama kivutio kikuu cha utalii duniani, huku akisisitiza utunzani wa mazingira ili rasilimali zilizopo zidumu.
“Kupitia mashindano ya urembo, washiriki kutoka nchi zaidi ya 140 watapata nafasi ya kuifahamu Tanzania , jambo ambalo litachochea utandawazi na umoja,” amesema.


