Na Winfrida Mtoi
MASHINDANO ya kuogelea kwa watoto ya ‘East Africa Development Swimming Gala’ yameanza kwa kishindo leo jijini Dar es Salaam, huku vipaji vilivyoonyeshwa na chipukizi hao vikiwakosha wadau na kuivuta Serikali ikiahidi ushirikiano wa kudumu.
Michuano hiyo iliyoandaliwa na Taasisi ya Prime Sports Agency, imeanza kurindima leo Aprili 18, 2026, katika bwawa la Shule ya Sekondari FK na inatarajiwa kufikia tamati kesho Jumapili.
Waogeleaji chipukizi wenye umri kati ya miaka 4 hadi 13 kutoka nchi za Uganda, Kenya, na wenyeji Tanzania, wameonyesha uwezo mkubwa katika siku ya kwanza, jambo lililomvutia mwakilishi wa Katibu Mkuu wa Baraza la Taifa la Michezo (BMT).


Akizungumza katika ufunguzi huo, mwakilishi wa BMT, Adam Tunga, amesema kuwa Serikali kupitia taasisi hiyo iko tayari kutoa sapoti ya hali na mali kwa waandaaji ili kuhakikisha vipaji hivyo vinaendelezwa badala ya kuishia njiani.
”Haya ni mashindano ya kipekee kwani ni mara ya kwanza kufanyika nchini yakihusisha watoto wadogo kwa kiwango hiki. Ni rika sahihi katika kutengeneza wanamichezo wa baadaye. Hatutaki kuona wanamichezo wakitokea kama miujiza, bali watengenezwe kitaalamu kama wanavyofanya TSA na mdau huyu aliyeanzisha mashindano haya,” alisema Tunga.
Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mchezo wa Kuogelea Tanzania (TSA), David Mwansyoge, ameipongeza Prime Sports Agency kwa kuleta maendeleo kwa vitendo na kueleza kuwa idadi ya washiriki inatia moyo.
”Lengo letu ni kukuza mchezo huu na kuwavuta Watanzania wengi zaidi. Leo tuna watoto 600, lakini malengo yetu ni kufanya magala mengi yatakayokusanya watoto zaidi ya 2,000. Tukiwa na idadi kubwa ya wataalamu, ushindani utaongezeka na kutupa fursa ya kufanya vizuri kimataifa,” alieleza Mwansyoge.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Prime Sports Agency, Lameck Borega, amesema kuanzishwa kwa gala hiyo ni sehemu ya kutekeleza maelekezo ya viongozi wa Serikali katika kuibua vipaji.
”Wiki chache zilizopita, Waziri mwenye dhamana ya michezo alitupa changamoto kwa nini Tanzania haina waogeleaji wengi wa ushindani. Tulilichukua hilo kama agizo na kuamua kulifanyia kazi kwa vitendo kupitia watoto hawa,” alisema Borega.
Borega aliongeza kuwa kutokana na mwitikio mkubwa wa wazazi na wadau waliojitokeza kushuhudia watoto wao, mashindano hayo sasa yatakuwa yakifanyika kila mwaka.


