Na Mwandishi Wetu
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ametembelea mradi wa Mji wa AFCON – 2027 Fumba uliopo Mkoa wa Mjini Magharibi, pamoja na kukagua uwanga unaotarajia kutumika kwa michuano hiyo
Ziara hiyo imefanyika leo Aprili 14, 2026, akiambatana na Waziri wa Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo, Dk. Riziki Pembe Juma, pamoja na wadau wa mradi wa AFCON Fumba.
Katika ziara hiyo, Rais Mwinyi amekagua maeneo mbalimbali ya uwanja huo, unaotarajiwa kutumika kwa michuano ya AFCON mwaka 2027 itakayofanyika kwa ushirikiano wa nchi tatu za Afrika Mashariki za Kenya, Uganda na Tanzania.

Aidha, ametembelea na kukagua miundombinu inayotarajiwa kujengwa kuzunguka uwanja huo, ikiwemo hospitali, barabara, migahawa, maduka makubwa (mall) pamoja na huduma nyingine muhimu zitakazouzunguka mji huo wa kisasa.
Uwanja huo unakadiriwa kuchukua watazamaji elfu 35, ukiwa na viwango vya ubora vinavyokubalika na Shirikisho la Soka Barani Afrika (CAF).


