Na Tatu Mohamed
MKUTANO Mkuu wa Kamati Tendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) unatarajiwa kufanyika Februari 13, 2026 katika ukumbi wa Hyatt Regency, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 9, 2026 na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Paul Makonda amesema kuwa uamuzi wa kufanyika kwa mkutano huo nchini umetokana na juhudi za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye Januari 16 mwaka huu alituma ujumbe maalumu kwa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF), Bw. Patrice Motsepe.

Amesema ujumbe huo ulikuwa ni sehemu ya kutambua mchango mkubwa anaoutoa Bw. Motsepe katika kuendeleza mpira wa miguu barani Afrika, hususan katika kuinua vipaji vya vijana na kuhimiza amani kupitia michezo.
Aidha, Waziri Makonda ameongeza kuwa katika ujumbe huo, Dkt. Samia alimweleza Rais wa CAF dhamira ya Serikali ya Tanzania kuwekeza kikamilifu kwenye michezo kwa gharama yoyote ili kuhakikisha nchi inakuwa kinara wa michezo barani Afrika na hatimaye duniani kwa ujumla.
“Mhe. Motsepe amepokea ujumbe wa Dkt. Samia kwa uzito mkubwa, na katika mazungumzo yetu tulijadiliana masuala mbalimbali, yakiwemo CAF kufanya mikutano yake ya mwaka hapa nchini Tanzania,” amesema Makonda.
Ameeleza kuwa ujio wa Rais wa CAF na Kamati Tendaji utampa fursa ya kujionea maendeleo na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan katika sekta ya michezo.
Waziri Makonda ameongeza kuwa tayari Rais Motsepe ameridhia kufanya mkutano huo nchini, na kwamba leo Februari 9, timu ya sekretarieti ya CAF imeanza kuwasili nchini kwa maandalizi ya mkutano huo utakaofanyika Februari 13, 2026.


