Na Mwandishi Wetu
TUME Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imetangaza ratiba ya kuchukua fomu za uteuzi kwa wagombea wa vyama 14 vya siasa waliopendekezwa kugombea nafasi ya Rais na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, zoezi linaloanza kesho Agosti 9, 2025.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma, Mkurugenzi wa INEC, Kailima Ramadhani, alisema kuwa kesho fomu zitachukuliwa na wagombea kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM), National Reconstruction Alliance (NRA) na Alliance for African Farmers Party (AAFP).
“Hadi leo tarehe 8 Agosti 2025, tumepokea barua kutoka vyama vya siasa 14 zikiainisha tarehe na muda ambao wagombea wao watakuja kuchukua fomu katika ofisi za Tume zilizopo Njedengwa, Dodoma,” amesema Kailima.

Kwa mujibu wa ratiba hiyo, vyama vitakavyofuata ni Chama cha MAKINI (10 Agosti), The National League for Democracy – NLD (10 Agosti), United Peoples’ Democratic Party – UPDP (10 Agosti), na African Democratic Alliance Party – ADA–TADEA (11 Agosti).
Vingine ni Union for Multiparty Democracy – UMD (11 Agosti), Tanzania Labour Party – TLP (11 Agosti), Chama Cha Kijamii – CCK (12 Agosti), Chama cha Ukombozi wa Umma – CHAUMMA (12 Agosti), Alliance for Democratic Change – ADC (12 Agosti), Democratic Party – DP (13 Agosti) na National Convention for Construction and Reform – NCCR–MAGEUZI (15 Agosti).
Kailima amesema Tume imeandikia vyama hivyo barua rasmi kuhusu ratiba ya utoaji fomu na kusisitiza kuwa orodha hiyo inahusu vyama vilivyowasilisha taarifa zao kufikia leo.
Amesema endapo vyama vingine vitajitokeza, ratiba mpya itaandaliwa.Amevitaka vyama kuendelea na maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2025 kwa kuzingatia katiba, sheria na kanuni za uchaguzi, huku akivipongeza kwa maandalizi yanayoendelea.


