Na Tatu Mohamed
WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umeibuka mshindi wa kwanza kwa jumla katika kundi la Uwezeshaji wa Biashara na Uwekezaji kwenye Maonesho ya 49 ya Biashara ya Kimataifa yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Nyerere, Dar es Salaam.
Tuzo hiyo imetolewa Julai 7, 2025 wakati wa hafla ya ufunguzi rasmi wa maonesho hayo iliyoongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Mwinyi.
Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Meneja wa Alama za Biashara wa BRELA, Seka Kasera ambaye pia alikuwa akikaimu nafasi ya Afisa Mtendaji Mkuu wa Wakala huo, aliwashukuru watumishi wenzake kwa kujitoa na kushiriki kikamilifu katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Tuzo hii si bahati nasibu. Watumishi wetu wamekuwa wakitoa huduma tangu siku ya kwanza ya maonesho na wateja wamekuwa wakimiminika kwa ajili ya kusajili biashara na kupata leseni,” alisema Kasera.
Alibainisha kuwa BRELA itaendelea kutoa huduma bora hata baada ya maonesho, na kuwahakikishia wananchi kuwa wanaweza kuendelea kupata huduma za usajili kwa haraka na kwa weledi.
“Tunaendelea kusajili papo kwa hapo hapa sabasaba. Hii ni fursa kwa wananchi wote kuja na kupata huduma bila usumbufu,” aliongeza.
Tuzo hiyo ni uthibitisho wa jitihada za BRELA katika kuwezesha mazingira bora ya biashara na uwekezaji nchini kupitia usajili wa haraka, uwazi na matumizi ya teknolojia.


