Na Mwandishi Wetu
Makamu wa Rais Dk. Philip Mpango na mwenza wake Mama Mbonimpaye Mpango wameungana na waumini mbalimbali wa Kanisa Katoliki Duniani kushiriki Dominika ya Ekaristi Takatifu katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Yohana wa Laterano lililopo Roma nchini Italia.
Misa hiyo imeongozwa na Papa Leo XIV. Makamu wa Rais yupo nchini Italia kumwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Ubia wa Maendeleo kati ya Afrika na Serikali ya Italia (Mattei Plan) pamoja na mikutano mbalimbali ya uwili.
Katika hatua nyingine Makamu wa Rais ametembelea Kampuni ya Kimataifa ya Uzalishaji wa Vifaa Tiba ya Health 3000 jijini Roma, Italia.

Katika ziara hiyo, Dk. Mpango amefanya mazungumzo na viongozi wa kampuni hiyo, wakiongozwa na Mwenyekiti Maurizio Flammini na Mkurugenzi Mtendaji, Eleonora Flammini. Mazungumzo yao yakilenga kuimarisha ushirikiano katika sekta ya afya, hususani kwenye matibabu kwa njia ya mtandao (telemedicine).
Health 3000 ni mojawapo ya kampuni zilizo chini ya FG Group, inayojikita katika uzalishaji wa vifaa tiba kwa kutumia teknolojia za kisasa.

Dk. Mpango yupo nchini Italia kumwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Ubia wa Maendeleo kati ya Afrika na Serikali ya Italia (Mattei Plan), pamoja na mikutano mingine ya ‘uwili’.


