Na Mwandishi Wetu
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Philip Mpango ametoa rai kwa wafamasia nchini kuendelea kulipa kipaumbele suala la elimu ya matumizi sahihi ya dawa ili kuisaidia jamii kutambua na kuepuka madhara ya matumizi holela ya dawa.
Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati wa wa Ufunguzi wa Kongamano la Kisayansi na Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Chama cha Wafamasia Tanzania leo Juni 4, 2025 unaofanyika jijini Arusha.
Amesema yamekuwepo matumizi mabaya ya dawa kwa baadhi ya wananchi, kama vile matumizi ya dawa pasipo kushauriwa na daktari, matumizi ya dawa za usingizi kama kilevi, matumizi ya dawa kunenepeshea mifugo pamoja na matumizi ya dawa kukoleza pombe za asili.

Halikadhalika, Makamu wa Rais amewasisitiza wanataaluma wote wa famasi kufanya kazi kwa kuzingatia kiapo na miiko ya taaluma yao. Ameliagiza Baraza la Famasi kusimamia kwa ukaribu suala hilo ili kuwahakikishia wananchi huduma bora.
Pia ametoa rai kwa vyuo vinavyofundisha taaluma ya famasi kuzingatia maadili katika ufundishaji ili kuzalisha wanataaluma wenye maadili, weledi na ujuzi stahiki.
Aidha, Makamu wa Rais amekemea tabia ya upotevu wa dawa kutokana na wizi, ambapo amesema badala ya dawa muhimu kupatikana kwenye vituo vya afya, hupatikana kwenye maduka binafsi ya dawa yanayomilikiwa na baadhi ya wafamasia. Amewataka wafamasia wanaojihusisha na tabia hiyo kuacha mara moja pamoja na kuviagiza vyombo vinavyohusika kuchukua hatua stahiki kwa wale watakaobainika kujihusisha na vitendo hivyo.
Vilevile, Makamu wa Rais amewasihi wanataaluma wa famasia kuongeza chachu ya kufanikisha mpango mahsusi wa Bima ya Afya kwa Wote kwa kuhamasisha wananchi kujiunga na Mfuko wa Bima ya Afya na kuhakikisha upatikanaji wa dawa zilizo salama na zenye ubora katika vituo wanavyofanyia kazi. Amesema lengo kuu la mpango huo ni kuhakikisha watanzania wote wanapata huduma ya dawa bila vikwazo.
Makamu wa Rais amesema Serikali inatambua na kuthamini mchango wa wafamasia katika utoaji wa huduma za afya na itaendelea kushirikiana na wataalamu hao ili kutoa huduma bora za dawa nchini.