Na Mwandishi Wetu, Dodoma
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan amewakumbusha Majaji na Mahakimu nchini kuwa kazi hiyo ni dhamana ambayo inataka uadilifu, na nidhamu na wasiwe kama ‘Miungu Watu’.
Rais Samia ameyasema hayo leo Februari 03, 2025 wakati akizindua shughuli za Mahakama kwa mwaka 2025, katika Siku ya Sheria nchini.
“Kazi ya kutoa haki ni kazi ya Mungu, ambayo mbali ya kutoa haki, ana kudra na jaala. Anaweza kuamua akupe au akunyime, sasa hiyo ni kazi ya Mungu,” amesema Rais Samia.

Amewasihi pia wanapoanza mwaka mpya wa Mahakama wazikague nafsi na dhamira zao, na wadhamirie daima kukaa upande wa haki na kutenda haki.
Rais Samia pia ameelekeza elimu ya sheria kutolewa kwa vyombo vya Serikali ili navyo vielimike, kwani elimu ya sheria inapaswa kutolewa sio kwa wananchi pekee bali hata kwa Serikali.

Hata hivyo Rais Samia amesema mwelekeo wa Tanzania katika miaka 25 ijayo ni kupunguza matumizi ya fedha taslimu mkononi na kupambana na mifumo ya fedha za kidijitali (Cryptocurrency), na kwamba katika hayo lazima nchi ijipange vizuri.
Naye, Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, amesema kuwa migogoro ya ardhi ndiyo chanzo kikuu cha jinai na changamoto nyingi za kijamii na kiuchumi nchini, hivyo inahitaji uangalizi wa hali ya juu katika Dira ya Taifa ya Maendeleo kufikia mwaka 2050.

Profesa Juma ameeleza kuwa migogoro ya ardhi inaathiri uwekezaji, biashara, mirathi na masuala mengine ya kijamii.
“Migogoro ya ardhi ni chimbuko la changamoto nyingi. Ikiwa tutaweka mifumo bora ya usimamizi wa ardhi, tutapunguza migogoro mahakamani, na mingi itaishia kwenye usuluhishi,” amesema Profesa Juma.
Awali Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Wakili Boniface Mwabukusi, amesema chama hicho kinaposhirikiana na Serikali haimaanishi kwamba wanalamba asali, na kwamba wao si kikundi cha magaidi.

“Tunapata changamoto watu wanapoona tukishirikiana na Serikali, wanafikiri tunalamba asali. TLS si kikundi cha magaidi, kwa hiyo sehemu ya kuonya tutaonya kwa haki, ya kupongeza tutapongeza kwa haki, ya kushiriki kufanya kazi tutashiriki pamoja, kulijenga Taifa letu na kumhudumia Mtanzania,” amesema Mwabukusi.

Hata hivyo, ametaja changamoto zinazoathiri taaluma hiyo nchini kuwa ni pale wanaposimamia kesi za watu wanaotuhumiwa kwa makosa makubwa, ikiwamo mauaji, na kusisitiza kuwa uwakili ni kazi.
