Na Mwandishi Wetu, Media Brains
Waziri wa Fedha, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema hadi kufikia Machi 2024, deni la Serikali limefikia Shilingi trilioni 90. Hata hivyo, amebainisha kuwa nchi bado iko imara kutokana na tathmini iliyofanywa na wataalamu wa ukaguzi wa madeni.
Akizungumza, Juni 13, 2024, wakati akiwasilisha Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2024/2025, Dk. Nchemba alisema kati ya deni hilo, Shilingi trilioni 60 ni deni la nje na Shilingi trilioni 30 ni deni la ndani.
Dk. Nchemba alisema uchumi wa dunia kuchafuka kumesababisha deni kuongezeka kwa zaidi ya Shilingi trilioni 5 bila kukopa mkopo wowote.
Ameeleza kuwa sababu nyingine za kuongezeka kwa deni ni mikopo ya zamani na mikopo mipya inayotumika katika ujenzi wa miundombinu ya barabara, reli ya kisasa, viwanja vya ndege, na miradi ya umeme. Pia, kupungua kwa thamani ya shilingi dhidi ya dola ya Marekani kutoka Machi 2021 hadi Machi 2024, ambapo imeshuka kutoka 2300 hadi 2500, imechangia ongezeko hilo.
“Madeni yanalipwa na yanapimwa. Mara kwa mara tunajadili ongezeko la deni bila kutaja sababu zake na fedha hizo zimetumika wapi. Ni kweli deni limeongezeka, lakini ni vizuri tukajielekeza katika kuelewa sababu za kuongezeka kwa deni na fedha hizo zimetumika wapi,” alisema Dk. Nchemba.
Amebainisha kuwa Serikali imekopa Shilingi bilioni 17,000 kutoka nje kugharamia miradi mbalimbali, ambayo imeongeza deni. “Tunatakiwa tujadiliane kama miradi tuliyofanya haikuwa na tija. Waliozoea kupita kwenye barabara nzuri wanaweza kuona umuhimu wa kukopa,” aliongeza.
Waziri huyo wa fedha alisema pia kuwa Serikali imetoa hati fungani maalumu yenye thamani ya Shilingi trilioni 2.17 kulipa mifuko ya hifadhi ya jamii kwa watumishi wa umma.
Kwa mwaka wa fedha 2024/2025, Serikali imepanga kukopa Shilingi trilioni 6.6 kutoka soko la ndani, ambapo Shilingi trilioni 4.2 zitatumika kulipa hati fungani zilizoiva na Shilingi trilioni 2.6 kugharamia miradi ya maendeleo.
“Watanzania wasitiwe hofu kuhusu masuala ya deni. Wataalamu wa ukaguzi wa madeni ambao wamefanyia tathmini nchi yetu wamesema bado iko imara katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC),” alisema Dk. Nchemba.
Kwa mwaka wa fedha 2024/2025, Serikali inatarajia kutumia Shilingi trilioni 49.35 kwa ajili ya matumizi, Shilingi trilioni 11 kwa mishahara, na Shilingi trilioni 2.17 kwa mfuko wa reli, barabara, maji, Rea na Tarura.