Na Mwandishi Wetu
TUME ya Uchunguzi wa matukio ya uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, inatarajiwa kuwasilisha ripoti yake rasmi kwa Rais Samia Suluhu Hassan, Aprili 23, 2026.
Taarifa kukabidhi ripoti hiyo imetolewa leo Aprili 21, 2026 Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Othman Chande, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za Tume.
Jaji Chande amesema jumla ya watu 63,603 wameifikia tume hiyo kutoa ushahidi wao kwa njia mbalimbali, ikiwemo kukutana ana kwa ana, kwa njia ya ujumbe mfupi wa maandishi na dodoso.
Amefafanua kuwa idadi kubwa ya ushahidi imepokelewa kupitia njia ya simu na ujumbe mfupi, ambapo watu 56,445 waliwasilisha taarifa zao kwa njia hiyo, watu 1,323, mashihidi wa viapo (Affidavit) watu 553, madodoso yenye maswali bila mtu kutaja jina lake ni 4, 891 na mikutano na makundi 202
Amesema kazi ya Tume hiyo imehusisha ukusanyaji wa ushahidi, maoni ya wadau mbalimbali pamoja na uchambuzi wa kina wa taarifa zilizokusanywa, ili kuhakikisha kuwa ripoti inayowasilishwa inakuwa ya kuaminika na yenye manufaa kwa Taifa.
Amesema ripoti hiyo itakayotolewa inatarajiwa kuwekwa hadharani kwa sababu ya maslahi ya umma na kuwezesha watu waone uhalisi wa nini kilitokea.
Tume hiyo ilizinduliwa Novemba 20, 2025 na Rais Samia kuchunguza undani wa sababu na chanzo cha matukio ya maandamano yaliyozaa vurugu siku ya Uchaguzi Mkuu.


