Na Winfrida Mtoi
NYOTA wa zamani wa Manchester United, Rio Ferdinand, ameeleza jinsi alivyovutiwa na fursa Tanzania, huku akiahidi kuwa taasisi yake itafuatilia vipaji vya timu ya Tanzania ya vijana chini ya miaka 17(Serengeti Boys) wakati wa Kombe la Dunia litakalofanyika Qatar ili kuona jinsi ya kutoa fursa kwa vijana hao.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Mei 22, 2026, wakati wa kuhitimisha ziara yake ya siku tatu nchini, aliipongeza Serengeti Boys kwa kufuzu Kombe la Dunia, alieleza kuwa hatua hiyo ni mafanikio makubwa yanayodhihirisha uwepo wa vipaji halisi nchini vinavyoweza kushindana kimataifa.
Kutokana na mijadala mbalimbali inayoendelea kuhusu ziara yake hiyo, amesema hajafika Tanzania kwa ajili ya siasa, bali kusaidia kuhamasisha vijana kupitia mchezo wa soka na atashiriki kusaidia vijana kupitia miradi ya maendeleo ya michezo na elimu.

Katika hatua nyingine nyota huyo ameweka wazi kuvutiwa na maendeleo ya Tanzania, utamaduni na fursa za kiuchumi, huku akisifiu uwekezaji wa miundombinu mbalimbali ikiwemo viwanja vya michezo, hasa maeneo yanayoandaliwa Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON).
“Tanzania ni nchi yenye fursa kubwa na maendeleo yanayoonekana wazi. Nimeguswa sana na ukarimu wa watu wa hapa na uzuri wa nchi hii. Ndio maana nimekubali kwa mikono miwili kuwa balozi wa utalii, ili nisaidie kuonyesha ulimwengu kile ambacho Tanzania imebarikiwa,” amesema Ferdinand.


