Na Mwandishi Wetu
MSANII wa filamu nchini, Hashim Kambi, amefariki dunia leo alasiri akiwa anapatiwa matibabu katika Hospitali ya Miko, jijini Dar es Salaam.
Taarifa za kifo cha Kambi zimethibitishwa na Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), Rajabu Amir, akiaeleza kuwa marehemu alipata changamoto ya kiafya ghafla alipokuwa katika majukumu yake ya kikazi.
Marehemu Kambi aliyekuwa akijulikana pia kwa jina la Ramsey ni mmoja wa wasanii wakongwe waliacha alama katika sanaa ya maigizo nchini kutokana na kuigiza filamu nyingi na kusaidia kukuza vipaji vichanga.
Miongoni mwa filamu alizoigiza ni Binti Yangu ambayo ni yake mwenyewe, nyingine ni Simu Ya Kifo, Binti Nusa, Babu Seya, Kipusa, The Lost Twins,Kipuri, Honey Moon, Surprise, Ripple of Tears, Miss Call na Romance.
Kabla ya kuingia katika sanaa ya uigizaji,marehemu Kambi aliwahi kucheza soka akiitumikia kilabu ya Yanga.

Wakati huo huo msanii wa muda mrefu wa Bongo Flava, Selemani Mvamba maarufu Spack, naye amefariki dunia leo 27 Aprili 2026 nyumbani jijini Dar es Salaam.


