Na Mwandishi Wetu
MKURUGENZI wa ufundi Shirikisho la Mpira wa Miguu kwa Watu wenye Ulemavu (TAFF), Shaban Msangi ameitembelea timu mpya ya soka kwa watu wenye ulemavu ya Unyanyembe mkoani Tabora ikiwa ni maandalizi ya Ligi Kuu Soka, itakayoanza Julai, 2026, jijini Dar es Salaam.
Msangi amesema kutembelea timu hiyo ni moja ya juhudi za shirikisho katika kukuza mchezo wa soka kwa watu wenye ulemavu kwa kuhakikisha wanaifikia mikoa mingi ili kupata idadi kubwa ya timu kuelekea katika ligi hiyo.
Hata hivyo amesema kuna changamoto wanayokutana nayo, kwa mfano katika timu hiyo ya Unyanyembe kuna uhaba wa vifaa vya michezo kama vile jezi, viatu na magongo na kuwaomba wadau kujitokeza kutoa sapoti.
“Kama tunavyojua mchezo huu ni kwa watu wenye ulemavu, ni watu wenye mahitaji maalum, ni mchezo ambao umebeba zaidi hisia za watu,” ameeleza Msangi.
Kwa upande wake kocha wa timu hiyo ya Unyanyembe, Hamad Simba amesema wanaendelea na mazoezi ya kujiandaa na ligi hiyo, huku akiwahimiza wakazi wa mkoa huo kupeleka vijana kujiunga na timu.
“Tuna nafasi bado vijana waliopo wilayani, popote pale mkoa wa Tabora waje wajiunge na timu nafasi bado ipo. Lakini pia ombi langu nikipata msaada wa vifaa itasaidia zaidi kujenga timu hii,” amesema.


